Monday, June 7, 2010

SEIF AWAONYA WANAOPINGA MARIDHIANO YA KISIASA ZANZIBAR

Katibu mkuu wa chama cha wananchi CUF Seif Sharif Hamad amesema anashangazwa kuona baadhi ya wazanzibari wanakula njama za kuwatenganisha wananchi baada ya kufikiwa maridhiano ya kisiasa.

Akizungumza katika sherehe fupi ya kurejesha fomu ya kugombea nafasi ya urais wa Zanzibar kupitia CUF amesema watu hao wanajaribu kuyabeza mafanikio ya maridhiano na kusema lengo lao ni kutaka Wazanzibari wahasimiane ili kulinda maslahi yao binafsi.

Hamad amesema mataifa ya nchi wahisani yamepongeza hatua iliyofikiwa na Zanzibar ya kufungua ukurasa mpya wa melewano ambapo nchi hizo zimeahidi kutoa misaada yao na kuwaonya wanaojaribu kuhujumu maridhiano hayo …

Aidha katibu mkuu huyo amewataka wananchi kuendelea kuunga mkono maridhiano ya kisiasa kwa kushiriki kwa wingi katika kura ya maoni inayotarajiwa kufanyika Julai 31 mwaka huu kwa kukubali mfumo mpya wa serikali ya mapinduzi Zanzibar.

Katibu mkuu wa CUF Hamad anakuwa mwanachama pekee wa CUF kutaka kuteuliwa na chama chake kugombea nafasi ya urais wa Zanzibar.

Mwaka 1995 wanachama wa CUF Mataka Amour Mataka na Suleiman Khamis walijitokeza kuchuana na kiongozi huyo, lakini baadae walijiondoa katika mkutano wa baraza kuu la chama hicho.

No comments:

Post a Comment