Friday, February 5, 2010

RADA YA TANZANIA YAIGHARIMU BAE

BAE Systems, mojawapo ya makampuni makubwa kabisa duniani ya uundaji wa vifaa vya kijeshi, itatozwa faini ya dola milioni 400.

BAE inalipa faini hiyo baada ya kukiri hatia ya kufanya njama ya kuwasilisha taarifa za fedha zenye udanganyifu mbele ya serikali ya Marekani.

Vile vile, imekubaliana na Idara ya Upelelezi wa Makosa Mazito ya Ugandanyifu ya Uingereza (SFO), kukiri kuwa na hatia ya kushindwa kutekeleza wajibu wake.

Wajibu huo ulikuwa ni kuweka kumbukumbu sahihi za mahesabu katika malipo yaliyofanywa kwa mshauri wake wa masoko nchini Tanzania ili kufanikisha mauzo ya rada ya kuongozea ndege.

BAE Systems imeagizwa na idara hiyo ya Uingereza, kulipa faini ya dola milioni 30, ambapo kati ya hizo, kiasi kitapelekwa Tanzania kusaidia shughuli za hisani.

Hata hivyo, hatua hiyo ni fedheha kubwa kwa BAE kutokana na kukiri kuwa na hatia ya mashtaka ya jinai Marekani na Uingereza.

Ingawa adhabu ya Uingereza inaonekana kuwa ndogo kuliko ile ya SFO iliyokuwa ikitaka, inaaminika kuwa ni rekodi ya kipekee kwa kampuni ya Uingereza kukutwa na hatia ya jinai.

Mashtaka ndani ya Uingereza yanahusiana na kampuni hiyo kuiuzia Tanzania rada ya kuongozea ndege kwa mamilioni ya dola katika mkataba wenye utata uliosaniwa mwaka 1999.

No comments:

Post a Comment