Thursday, July 15, 2010

RAIS MUSEVEN ATAKA MAJESHI ZAIDI SOMALIA

Rais Yoweri Museveni wa Uganda ameelezea haja ya kuimarishwa kwa majeshi ya Afrika ya kulinda amani nchini Somalia na kufikia wanajeshi elfu 20 ili kuwateketeza wale wote waliyohusika na mashambulio ya mabomu mjini Kampala ambapo watu zaidi ya 70 waliauawa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika mji wa Ntungamo magharibi mwa Uganda, Rais Museveni amesema kuwa nchi yake inaweza kushiriki katika mpango huo wa kuwa na wanajeshi elfu 20 ambao watashirikiana na serikali ya mpito kuwateketeza magaidi.

Amesema mataifa ya Afrika Mashariki yamekubali kutuma wanajeshi wa ziada elfu mbili nchini Somalia, lakini baada ya tukio la Jumapili mjini Kampala,Rais Museveni amesema wanajeshi zaidi wanahitajika.

Kundi la Al Shaabab limedai kuhusika na shambulio hilo la mabomu na limetishia kufanya tena mashambulio kama hayo nchini Burundi.Burundi na Uganda ndiyo pekee zenye wanajeshi katika kikosi cha wanajeshi elfu sita cha Afrika cha kulinda amani nchini Somalia AMISOM.

Wakati huo huo kiongozi wa kundi la al-Shaabab Sheik Muktar Abu Zubayr amesema mashambulio hayo ya Uganda ni mwanzo tu na kwamba mashambulio zaidi yatafuatia.

No comments:

Post a Comment