Tuesday, July 6, 2010

NIGERIA YAFYATA MKIA MBELE YA MKWARA WA FIFA

Hatimaye uongozi wa Serikali ya Nigeria umefikiria upya na kubadili uamuzi wake ulioutoa awali kuhusu kuizuia timu ya taifa ya soka ya nchi hiyo "Super Eagles" kutokushiriki katika michezo yoyote ya Kimataifa kufuatia kuvurunda katika michuano ya kombe la dunia 2010 inayoendelea huko nchini Afrika Kusini.

Awali, raisi wa Nigeria, Goodluck Jonathan alisema timu hiyo imeonesha kiwango duni katika mashindano na kufuatia majadiliano na viongozi wengine, ilionekana njia ya kuchukua kwa sasa ni kwa kuizuia isishiriki mashindano yoyote ikiwa ni pamoja na kuwafukuza viongozi wa shirikisho la soka nchini Nigeria, (Nigeria Football Federation - NFF), taarifa ambazo hazikupokewa vizuri na shirikisho la mpira wa miguu duniani, FIFA, ambao walituma waraka kwa uongozi wa Serikali ya Nigeria kuwataka kubatilisha uamuzi huo au kupata adhabu ya FIFA.

Kabla ya kuisha kwa muda wa waraka wa FIFA kwa Serikali ya Nigeria, ndipo ilipotangazwa kuwa baada ya kujadiliana na kuona kuwa uamuzi wa kuifungia timu hiyo utawanyima fursa mamilioni ya vijana chipukizi wanaocheza mchezo huo na pia kuwavunja moyo watoto wanaopenda soka, raisi wa Nigeria ametangaza kufuta uamuzi wake wa awali na anabaliana na FIFA kwa maslahi ya wachezaji chipukizi na Taifa kwa ujumla.

Kwa kawaida, nchi yoyote inayokubali kushirikiana na FIFA katika mchezo wa mpira wa miguu, Serikali haipaswi kuingilia baadhi ya maamuzi yanayohusu mchezo huo isipokuwa katika masuala machache kadiri ya muongozo wa katiba. Vyama vya michezo hutakiwa kuachwa huru na hupokea maagizo toka FIFA pekee.

No comments:

Post a Comment