Monday, February 15, 2010

KIBAKI ABATILISHA UAMUZI WA RAILA

Hali tete ya serikali ya muungano ya Kenya imeendelea kudhihirika huku Rais Mwai Kibaki akibatilisha uamuzi wa awali wa waziri mkuu Raila Odinga wa kuwasimamisha kazi mawaziri wawili kuhusiana na uchunguzi wa kashfa za ufisadi.

Awali Waziri mkuu Raila Odinga alitangaza kuwasimamisha kazi waziri wa kilimo William Ruto na waziri wa elimu Prof Sam Ongeri, akisema alifanya hivyo baada ya ripoti mbili za uchunguzi wa mashirika mawili tofauti kuonyesha kwamba mawaziri hao wanastahili kuchunguzwa zaidi.

Kashfa hizo zinahusu mahindi yanayosemekana kuuziwa wafanyabiashara kwa njia ya ufisadi badala ya kuwauzia wananchi, na nyingine ni kuhusu ubadhirifu wa mamilioni ya pesa zilizokusudiwa kugharamia elimu ya bure.

Taarifa kutoka Ikulu imeeleza kwamba Rais Mwai Kibaki amebatilisha uamuzi huo kwa kuzingatia kipengee cha mkataba wa serikali ya muungano, kinachohitaji kuwepo mashauriano na kiongozi wa chama kabla ya waziri yeyote kufutwa kazi.

''Kuondolewa kwa Waziri yeyote aliyeteuliwa na chama cha siasa katika serikali ya muungano utafanywa pale tu na baada ya mashauriano na makubaliano kimaandishi kwa kiongozi wa chama.'', taarifa hiyo ilisema.

Lakini Bw Odinga ameambia BBC kwamba kulingana na mwafaka wa serikali ya mseto , mashauriano yanahitajika tu katika kuteua au kumwachisha kazi waziri na sio katika kumsimamisha kazi.

Amesema alichokifanya yeye ni kuwaambia mawaziri wahusika kukaa kando ili uchunguzi ufanyike kuhusiana na kashfa hizo na kwamba hajamwachisha kazi waziri yeyote.

Bw Odinga amesema Rais Kibaki amevunja sheria na katiba kwa kubatilisha uamuzi wake.

No comments:

Post a Comment