Monday, July 26, 2010

MOURINHO AMTAKA ASHLEY COLE

Kocha mpya wa timu ya Real Madrid Jose Mourinho ametangaza dau la Pound milioni 20 kwa mlinzi wa kushoto wa timu ya Chelsea Ashley Cole.

Mourinho alimshauri meneja wa Real Madrid Jorge Valdano huko Bernabeu kwamba wajaribu kutangaza dau hilo kwa timu ya Chelsea au kama itashindikana basi hata kwa kuingia mkataba wa kubadilishana na mchezaji ambapo Mourinho alimtaja kiungo mshambuliaji raia wa Uholanzi Rafael van der Vaartambae ndie atakae ingia katika mkataba wa kubadilishwa na Cole.

Vyanzo kutoka Real vimeeleza kwamba Mourinho anataka wachezaji ambao wana uzoefu kwa hivyo Ashley cole anafaa.
Kwa upande wake kocha wa timu ya Chelsea Carlo Ancelotti mpaka sasa ameonesha kutokubaliana na Mourinho kwa kumuuza Cole "kama mchezaji hajaridhika nitatumia njia ambayo itaweka mambo sawa lakini nafikiri Ashley atabaki kwa sababu hajawahi kusema kwamba hajaridhika" alisema Ancelotti.
Soma Zaidi ...
Soma Zaidi ...

UCHUNGUZI WA VIFO DUISBURG WAANZA


Waendesha mashitaka nchini Ujerumani, wameanza kuchunguza chanzo cha vifo vya watu 19 katika msongamano uliosababisha kukanyagana uliotokea kwenye tamasha la muziki la Love Parade katika mji wa Duisburg. Watu 342 walijeruhiwa katika msongamano huo uliotokea siku ya Jumamosi.

Akizungumza na waandishi habari katika mji wa Bayreuth, Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel alisema lazima uchunguzi wa kina ufanyike kubaini kilichosababisha maafa hayo.

Hapo jana gazeti la Ujerumani la Spiegel liliripoti katika mtandao wake kuwa waandalizi wa tamasha hilo walipewa kibali cha kuruhusu watu 250,000 kuhudhuria badala ya milioni 1.4 ambao walihudhuria. Mwandalizi wa tamasha hilo, Rainer Schaller alisema tamasha hilo halitafanywa tena kwa heshima ya wahanga wa maafa hayo na familia zao.
Soma Zaidi ...

Sunday, July 25, 2010

Asilimia 23 ya watu wazima Lesotho na Msumbiji ni waathirika wa maradhi ya Ukimwi.

Mkutano wa 18 wa kimataifa wa ukimwi unafungwa rasmi hii leo mjini Vienna Austria,huku suala la msongamano wa wafungwa magerezani,likitajwa kuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa maradhi hayo.

Mkutano huo pia umejadili masuala kadhaa juu ya jinsi ya kukabiliana na ugonjwa huo,ambao umegeuka tishio zaidi duniani.

Tatizo la msongamano wa wafungwa na mahabusu magerezani,limetajwa kuwa ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya kusambaa kwa ugonjwa huo,lakini pia Mkutano huo umeelezwa kuwa uchangiaji wa sindano na michoro ya alama za tattoo kuwa nayo yanachangia kusambaa kwa virusi hivyo.

Kwa mujibu wa wataalamu wa kitengo cha ofisi ya umoja wa mataifa kinachoshughulikia madawa ya kulevya na uhalifu,wameeleza kuwa zaidi ya watu milioni 30 duniani,wameambukizwa maradhi hayo kutokana na matatizo ya msongamano wa magereza,huku matukio ya kuwepo kwa vitendo vya ngono na ulawiti vikitajwa kuchangia zaidi hali hiyo,kutokana na kukosekana kwa mipira ya kondomu.

Katherine Todrys aliyesimamia utafiti wa shirika la haki za binaadamu la Human right Watch,katika magereza 6 ya Zambia,ameeleza kuwa nchi hiyo imeshindwa kabisa kuwa na mkakati maalumu wa kuwapima wafungwa afya zao.

Mkutano huo umeelezwa kuwa hali ni mbaya zaidi nchini Zambia,ambapo watumishi 14 wa afya,wanahudumia zaidi ya wafungwa 15,300,katika magereza 86 nchini humo,na kueleza kuwa dawa pekee inayopatikana kwa wafungwa hao ni ya kutuliza maumivu na inayopunguza homa,hali inayohatarisha afya za wafungwa,hasa walioathirika na virusi vya Ukimwi.

Kwa mujibu wa ripoti iliyochapishwa na serikali ya Marekani mwaka 2008,imetaja kuwa zaidi ya asili mia 27 ya wafungwa nchini Zambia ni waathirika wa Ukimwi,ikiwa ni mara mbili ya wale walio nje ya magereza.

Kwa upande wa Nigeria,wanaharakati kutoka asasi ya uzazi wa mpango,wameeleza kuwa wanakabiliwa na hali ngumu katika kusambaza mipira ya kondomu,kutokana na imani za walio wengi,kuamini kuwa kitendo hicho ni sawa na kuchochea vitendo vya ngono.

Wakati huo huo,imeelezwa kuwa kutoa matibabu kwa kutumia timu ya wanajamii waishio vijijini kwa wagonjwa wapya wa ukimwi barani Afrika,ndio suluhisho pekee la kukabiliana na maradhi hayo,tofauti na kutegemea madaktari.

Imeelezwa kuwa timu ya wanajamii waishio vijijini,wanaweza kusaidia kupunguza gharama,na kuwasaidia waathirika wa Ukimwi,kuishi muda mrefu zaidi,kuliko wale ambao wanachelewa kupatiwa matibabu hayo,kwa kutegemea madaktari kutoka maeneo ya mbali.

Kitengo cha utafiti cha MSF;kilichofanya utafiti huo nchini Msumbiji na Lesotho kimefahamisha kuwa asilimia 23 ya watu wazima ni waathirika wa maradhi ya Ukimwi.

Daktari Helen Bygrave wa Medisins San Frontieres,MSF nchini Lesotho,amesema kuwa kati ya waathirika 1,128 wanaoishi maeneo ya vijijini nchini humo,asilimia 70 kati ya hao,wana uwezekano mkubwa wa kufariki katika kipindi cha miaka 2 ijayo,kuliko waathirika ambao waliwahi kupatiwa huduma ya matibabu kabla yao.

Ugonjwa wa ukimwi kwa mara ya kwanza uligunduliwa mwaka 1981 na kwamba kabla ya kuanza kutumika kwa dawa hizo za kupunguza makali ya ugonjwa,watu walianza kuugua ugonjwa huo ndani ya kipindi cha miaka kumi toka kupata maambukizo na hufariki baada ya mwaka mmoja au miwili.

Mkutano wa 18 wa kimataifa kuhusu ukimwi,umehudhuriwa na wataalamu wapatao 25,000, wakiwemo kutoka sekta za afya na watunga sera, ili kujadiliana hatua mbalimbali katika mapambano dhidi ya ukimwi na kuangalia njia za kuweza kutoa kinga zaidi na matibabu dhidi ya virusi vinavyosababisha ukimwi.

***DW - Deutsch Welle
Soma Zaidi ...

IJTIMAI ZANZIBAR - 2010

Salma Said,

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Amani Abeid Karume ametoa wito kwa Waislamu na wananchi wote wa Zanzibar kuunga mkono kura ya maoni kwa lengo la kuendeleza amani, mshikamano na kutofarikiana miongoni mwao kama Uislamu unavyosisitiza.

Rais Karume aliyasema hayo leo huko katika Msikiti wa Markaz Kuu Fuoni Migombani katika horuba yake aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa Ijtmai ya 17 ya Kimataifa na kusisitiza kuwa zoezi la kura ya maoni linalotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu ni ishara tosha ya kujenga umoja na mshikamano na hakuna sababu ya kukataa kwani sio jambo baya.

Katika hotuba yake hiyo, Alhaj Karume alisema kuwa Umoja wa Wazanzibari utafungua ukurasa mpya na kueleza kuwa dini ya Kiislamu imekuwa ikisisistiza amani na mshikamano miongoni mwa Waislamu hatua ambayo imefikiwa kwa kiasi kikubwa hapa Zanzibar hivi sasa.

Alhaj Karume alisema kuwa ni kawaida kila inapofika katika kipindi kama hichi Zanzibar kugubikwa na shughuli za kisiasa ambazo wakati mwengine hotukezea mambo ambayo hayana maslahi kwa wananchi lakini katika kipindi hichi mafanikio makubwa yamepatikana.

Alieleza kuwa hatua hiyo imefikiwa kutokana na maridhiano yaliofanyika kati yake na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad kwa kuangalia mustakbali wa nchi na wananchi wake hatua ambayo imeweza kuungwa mkono na wananchi walio wengi.

Rais Karume alieleza kuwa anafarajika kuona na kusikia Waislamu nchini pamoja na wananchi kwa jumla wakiunga mkono maridhiano hayo na kusisitiza kuwa sifa na hongera anazopewa kwa kuweza kuifikisha Zanzibar katika medani na amani na utulivu si zake pekee bali ni za wananchi wote wa Zanzibar.

Alhaj Karume alisisitiza kuwa umoja, amani na utulivu ndio msingi wa maendeleo na jambo hilo sio jipya kwa Zanzibar na kueleza kuwa umoja ni miongoni mwa Sera za Chama Cha Mapinduzi..

Rais Karume alitoa shukrani kwa maandalizi ya Ijtmai hiyo ya 17 sanjari na hatua nzuri za ujenzi zilizofikiwa na kuahidi kutoa ushirikiano wake kwa kuahidi changamoto zilizopo zinapatiwa ufumbuzi ikiwemo ujenzi wa barabara inayoelekea Markaz hiyo inajengwa kwa kiwango cha lami, kuwapatia usafiri na kuwatafutia viongozi wa Markaz nafasi za Hijja.

Aidha, Rais Karume alieleza kuwa lengo la serikali la kujengwa Chuo Kikuu cha Kiislamu lipo pale pale na juhudi zimekuwa zikichukuliwa katika kuhakikisha linafanikiwa na kuwaondosha hofu wale wanaodhani kuwa vyuo vya Kiislamu huwa vinatoa elimu ya msimamo mkali.

Nao Waislamu nchini wameleleza kuridhishwa na maridhiano yaliofanyika kati ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj. Dk. Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad na kueleza kuwa hatua hiyo ni maamrisho ya Allah ya kuimarisha umoja na kutofarikiana.

Akisoma hotuba fupi ya makaribisho, Mwenyekiti wa Jumuiya za Markazi Kuu ya Fuoni Amir Ali Khamis alisema kuwa leo ni siku ya faraja kubwa na furaha isiyokifani kwa Waislamu na wananchi wa Zanzibar wapenda Amani na Utulivu na salama nchini.

Amir Khamis alitoa wito kwa Waislamu wote na wananchi wote kwa ujumla kuunga mkono kwa dhati kabisa maridhiano hayo kwa faida ya Waislamu na Wazanzibar wote..
Alieleza kuwa Wazanzibari na Waislamu wa Zanzibar wamechoka na hasama na mabalaa yasiyokwisha kila panapoingia uchaguzi nchini “Tunatoa wito kwa Wazanzibari wote kuyapokea maridhiano haya kwa mikono miwili”,alisema Amir.

Nae Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, akitoa salamu zake kwa Waislamu waliohudhuria katika Ijtmai hiyo alieleza kuwa ni faraja kuwa kwa wananchi wa Zanzibar chini ya uongozi wa Alhj Karume wanakaa pamoja na kushirikiana kama dini inavyotaka.

Alisema kuwa hatua hiyo inaonesha dalili za umoja ziko wazi wazi kabiza na kusisitiza umuhimu wa kura ya maoni mwishoni mwa mwezi huu kwa wananchi wote kushiriki kikamilifu kwa kuunga mkono kwa kukubali umoja huo.

Akitoa hotuba ya Sala ya Ijumaa. Sheikh Othman Maalim alieleza kuwa maridhiano ya viongozi hao yanatokana na maarisho ya Mwenyezi Muungu ya kuwataka waumini kushikamana na kutofarikiana.

Maelfu ya Waumini kike kwa kiume wadogo kwa wakubwa, Masheikh na Maulamaa kutoka nchi mbali mbali zikiwemo za Afrika pamoja wa Waumini wenyeji wa Unguja na Pemba na Mikoa ya Tanzania Bara wamehudhuria katika Ijtmai hiyo ya siku tatu.

Soma Zaidi ...

Saturday, July 24, 2010

UMOJA WA AFRIKA KUPELEKA ASKARI ZAIDI

Jeshi la Umoja wa Afrika linalopambana na waasi wa Somalia wanaohusiana na Alkaida litaimarishwa kwa vikosi kutoka Guinea na kufikia idadi ya askari alfu 10.

Taarifa hiyo imetolewa kwenye kikao cha mawaziri wa nchi za Umoja wa Afrika wanaokutana mjini Kampala kabla ya kikao cha kilele cha viongozi wa Umoja huo.

Kwa sasa Umoja wa Afrika una askari kutoka Uganda na Burundi waliopo nchini Somalia.

Na Rais wa tume ya Umoja wa Afrika Jean Ping amewaambia wandishi habari mjini Kampala kwamba Djibouti nayo ipo tayari kuchangia majeshi.

Kuhusu Guinea bwana Ping amesema nchi hiyo inataka sana kupeleka majeshi nchini Somalia.

Mkutano wa nchi za Umoja wa Afrika unafanyika katika mji mkuu wa Uganda Kampala wiki mbili baada ya magaidi kufanya mashambulio katika mji huo na kuwaua watu 76 waliokuwa wanatazama fainali ya kombe la dunia.

Al Shabaab kundi linalohusiana na Alkaida lilisema kuwa lilifanya shambulio hilo. Soma Zaidi ...

Friday, July 23, 2010

Tangazo maalum kwa wazanzibari wote

Soma Zaidi ...

KOSOVO HAIJAKIUKA SHERIA YA KIMATAIFA

Mahakama ya Haki ya Umoja wa Mataifa imesema hatua iliyochukuliwa na Kosovo kujitenga na Serbia haijakiuka sheria ya kimataifa. Jaji Mkuu wa mahakama hiyo ya kimataifa iliyoko The Hague, Uholanzi, Hisashi Owada, alitoa uamuzi huo usio na mafungamano ambao huenda ukawa na athari zake miongoni mwa makundi yanayopigania kujitenga kote ulimwenguni. Kosovo imekuwa inatambuliwa na mataifa 69 kama nchi huru, ikiwemo Marekani na mataifa mengi ya Umoja wa Ulaya.

Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya, Catherine Ashton ameupokea kwa furaha uamuzi huo akisema kuwa umoja huo uko tayari kuzisaidia Serbia na Kosovo kufanya mazungumzo ya kuimarisha nguvu zao za kujiunga na umoja huo. Rais wa Serbia Boris Tadic alisema kuwa nchi yake haitabadilisha sera zake kuelekea Kosovo na serikali sasa inazingatia kuchukua hatua zaidi. Serbia na Urusi ziliyaongoza mataifa mengine kadhaa kutoitambua Kosovo kama taifa huru. Soma Zaidi ...

Thursday, July 22, 2010

JINSI WENZETU WANAVYOJALI

Tukiangalia hii picha tutaona ni jinsi gani hawa wenzetu wazungu wanavyojali usalama wa mtu, hii sehemu tiles zake zilivunjika na wakazitoa lakini kwa kua bado hii sehemu hawajaitengeneza basi idara husika wameweka kizuizi ambacho kinamkinga mtu asije akakanyaga kwa bahati mbaya akaumia, lakini sisi nchini kwetu utakuta shimo kabisa liko kati kati ya barabara na hakuna ishara yoyote ambayo idara husika itaiweka kusudi iweze kumuonesha mtu kama pale pana jambo fulani la hatari, mpaka watu tu wenyewe wafanye kusaidiana kwa kuweka kitu kama majani ya mti, kwa kweli tuko mbali sana katika safari yetu.
Haya ndio mambo ya nyumbani wahusika hawana hata habari Soma Zaidi ...

Wednesday, July 21, 2010

Nyota wa Bayern "Ribery" ahojiwa na polisi


Mchezaji nyota wa soka wa kimataifa wa timu ya Bayern Munich,Frank Ribery, alizuiliwa na maafisa wa polisi hapo jana na kuhojiwa , akishukiwa kushiriki katika kitendo cha ngono kwa malipo na kahaba mwenye umri mdogo.

Ribery na mwenzake Karim Benzema, walihojiwa kwa muda wa masaa kadhaa katika makao makuu ya polisi mjini Paris. Kesi hiyo ilijulikana hadharani mwaka huu baada ya msichana mmoja mwenye umri mdogo, kujitokeza na kusema kuwa wachezaji kadhaa wa timu ya taifa ya Ufaransa walimlipa kufanya naye kitendo cha ngono. Hatahivyo uchunguzi wa kesi hiyo uliahirishwa ili usiingiliane na matayarisho ya Ufaransa kushiriki katika mashindano ya kombe la dunia. Wakili wa Ribery amesema nyota huyo wa Bayern, hakujuwa kuwa msichana huyo ana umri wa chini ya miaka 18. Soma Zaidi ...

KILA MTU ANA HAKI YA KUOGELEA NA KUFURAHI

Soma Zaidi ...

SAMAKI WA NDUARO WALIEVULIWA NUNGWI

Wachukuzi wa samaki katika marikiti kuu ya samaki darajani wakimshusha samaki aina ya nduaro aliyevuliwa kijiji cha nungwi ambaye ameuzwa shillingi 1,500,000 katika soko la Nungwi.
Mchuuzi wa samaki marikiti kuu Darajani akimkata mapande samaki aina ya nduaro kwa ajili ya kuuzwa sokoni hapo samaki huyu anakadiriwa kufika zaidi ya tani mbili.

Wadau mlio ughaibuni mmeona hygiene - jinsi tunavyohakikisha hatupatwi na vijidudu vinavyosababisha maradhi licha ya Nduaro kushughulikiwa chini ambako hali yake ya usafi kama unayoiona. Kwani hata pweza kwanza lazime apate kichapo cha kupigwa na chini ili aregee na chini kwenyewe ni sehemu yoyote. Kisha huoshwa tayari kwa mapishi. Othman Mapara Soma Zaidi ...

Ng’o sitopiga Hapana

Na. B.OlE

Naikumbuka Zanzibar nzuri ambayo imenilea, kunitunza kwa utulivu na amani. Maumbile mazuri ambayo macho yangu yalipofungua kutoka kwa mama mzazi yalinilaki na kunipongeza huku yakanikaribisha kwa bashasha na furaha nyingi.

Mazingira yenye harufu ya manukato yenye kuleta kila ainaya furaha na faraja. Zanzibar iliokuwa njema, amani, utulivu, upendo na ukarimu.

Zanzibar iliokuwa na watu wapole, wasomi, wenye mapenzi, haiba na furaha na bashasha wakati wote.

Zanzibar ilioungana huku wazee wakiwa wamebarizi kwenye sehemu zao wakiangalia vijana wao wakicheza kwa mbwembwe na furaha tele.

Zanzibar ambayo ugomvi, ubaguzi, ilikuwa ni mwiko na sumu kali miongoni mwa jamii.

Zanzibar ambayo bahari yake ilishuhudia majahazi na mitumbwi ikipishana kutoka kisiwa kimoja kwenda chengine kwa nyimbo na hoi hoi huku watu wakufurahia udugu pamoja na usahiba wao.

Zanzibar ambayo upepo wa pwani ulitawala kuleta hali nyororo yenye kukidhi haja ya viumbe huku ndege na wao wakiimba kwa furaha kufurahia Amani ya visiwa vyetu.

Zanzibar ambayo hata misitu haikurudi nyuma kuashiria manyunyu na rasha rasha za mvua za miongo za hapa na pale.

Zanzibar ambayo mbara mwezi ilimwilika huku watoto wakicheza kinyuli nyuli nyulika mwanangu mwana jumbe kavaa nguo mbili ya tatu kajibandika…….

Zanzibar ambayo matunda na vyakula mbali mbali yalioteshwa na kuwafanya watu kuwa na siha na furaha ya maisha yao.

Maumbile haya mazuri na yenye kuvutia machoni mwa kila mtu kwa tabasamu yaliniahidi kunitunza na kunipa kila aina ya maisha bora na ya furaha kabisa.

Najiuuliza haya yote yameenda wapi, mbona nimekuwa mkiwa ? Mama yangu Zanzibar amekuwa Mgonjwa na mimi mtoto sina furaha wala bashasha.

Sitosahau ihsani na fadhila ya nchi yangu ndio maana nikasema Ng’o sitopiga HAPANA kura ya maoni.

SABABU ZANGU MAALUM:-

1.Kusema Hapana ni kuisaliti nchi yangu, mama alonilea.

2.Ni kuitakia mabaya na kutoijali nchi ilionilea kwa mapenzi makubwa.

3. Nitakuwa nimechangia kupoteza ile hidaya muhimu kwa visiwa vyetu , yaani utulivu na amani.

4.Nitakuwa nimeshiriki kikamilifu kuendeleza chuki, uhasama na ugomvi wa wananchi wenzangu bila faida yeyote ile.

5. Nachelea kuja kuulizwa siku ya malipo juu ya mchango wangu wa kusaidia machafuko Zanzibar, sitokuwa na jibu siku hiyo.

6. Kumsaliti mlezi alienipokea kwa mikono miwili ni kosa kubwa kiasi ambacho nitatakuja kustahiki adhabu kali hapo baadae na laana ya mola inaweza kinishukia.

7.Kuwapinga walio wengi wanaoitakia Zanzibar mema na maslahi kwa wananchi wote ni kitendo kisichokubalika katika jamii ya wastaarabu.

8.Kwenda kinyume na maamrisho ya dini yetu yenye kuhimiza amani na upendo miongoni mwetu ni kosa kubwa.

9.Kuwanyima fursa muhimu kwa Wazanzibar kuondosha tofauti zao za siasa za chuki zilizodumu kwa muda mrefu sasa ni jambo lisilokubadilika abadan.

10.Kutowatakia mema kwa kizazi kipya na kuwarithisha chuki na uhasama kwa watoto wetu sio jambo la kufurahia.

11.Kuwapa nguvu wale wote wanaopinga umoja na ushirikiano miongoni mwa Wazanzibar sio busara na maadili mazuri.

12. Kufurahia kila baada ya miaka mitano kuona Wazanzibar wakiteseka na kudhalilishwa bila sababu na hatimae kuuwana ni kujidhalisha kwa nafsi na hukumu yake itakuwa nzito.

13. Kutesana wenyewe kwa wenyewe wakati sote ni watu wa asili moja ni jambo la kuhuzunisha sana.

14.Kufurahia kuwaona wengine wakibaguliwa kwa rangi,kabila na sehemu wanazotoka jambo ambalo hata Mola wetu halifurahii, mimi kama kiumbe sitaki niwe nimeshiriki kwa hilo.

15.Kutengana na kurudisha nyuma maendeleo ya Taifa letu ni kwanyima fursa wengine hasa kizazi kipya.

16. Kuleta migawanyiko ndani ya jamii na kuwafanya wengine waonekane wana haki zaidi juu wenzao jambo ambalo litapelekea mgawanyiko na mifarakano ndani ya jamii.

17.Kukaribisha na kuwafanya watu wachache wasimame juu ya sheria huku walio wengi wakionewa na sheria hizo hizo haikubaliki.

18. Kuwafanya wachache wafaidi matunda ya nchi yetu huku walio wengi wakipata shida na kuteseka na familia zao ni uchoyo mbaya.

19.Kupoteza muelekeo wa Dola yetu ya Zanzibar na kupoteza kila kilicho chetu, na hatimae kuwa ni watu tusiokuwa na kwetu, hili halikubaliki.

20.Kukaribisha mabaya na kuunda misingi ya chuki na fitina zisizo kwisha na kugawa matabaka miongoni mwetu, sitoridhia.

21.Kuwaunga mkono wale vibaraka, mafisadi, wahafidhina,wanafiq wasioitakia mema Zanzibar na Wananchi wake, ni kutoipenda nchi yangu.

KURA yangu sitopiga Hapana ng’o, wewe jee?
Soma Zaidi ...

Tuesday, July 20, 2010

CHELSEA: "DROGBA HATUUZI"

Mabingwa wa soka nchini Uingireza timu ya Chelsea, wametangaza kwamba mshambuliaji wao machachari Didier Drogba hatauzwa.

Timu hio ya Chelsea wametangaza hayo baada ya wakala wa mchezaji huyo Thierno Seydi kusema kwamba kuna uwezekano wa Drogba kuuzwa kwa timu ya Manchester City.

Wakala huyo alisikika katika kituo kimoja cha radio akisema kwamba Drogba ataondoka Chelsea kwenda City kabla ya kipindi cha uhamisho kumalizika, kitendio ambacho kimepelekea Chelsea kutoa tamko.

Timu ya Machester City ilimtaka Drogba kwa msimu ujao wa ligi lakini hadi sasa imeshindikana kwa mchezaji huyo kuondoka Stamford Bridge, katika msimu wa ligi uliomalizika Drogba mwenye umri wa miaka 32 aliweza kupachika mabao 29 katika ligi kuu nchini Uingereza. Soma Zaidi ...

BAADHI YA TIMU ZINAZOSHIRIKI LIGI KUU UINGEREZA ZAPIGA MARUFUKU VUVUZELA


Timu sita nchini Uingereza ambazo zinashiriki ligi kuu nchini humo zimepiga marufuku kwa mashabiki kuingia katika viwanja vyao huku wakiwa na matarumbeta al-maarufu " vuvuzela".

Timu za Arsenal na Tottenham ndizo timu za mwanzo kupiga marufuku mavuvuzela kuingia katika viwanja vyao huku zikifuatiwa na timu za Liverpool,Sunderland, Birmingham na Westham.

Kwa upande wa timu ya Tottenham wameeleza sababu kuu ya kupiga marufuku vuvuzela ikiwa ni pamoja na usalama uwanjani hapo, wamesema kwamba ikiwa watu watashangiria kwa kutumia vuvuzela kuna uwezekano mkubwa wa watu kushindwa kusikia matangazo yatakayotolewa iwapo itatokezea ajali uwanjani hapo.

Katika sababu zilizotolewa na timu nyengine ni kwamba iwapo wataruhusu ushangiriaji wa vuvuzela wanaweza wakapoteza kawaida na desturi za ushangiriaji katika viwanja vyao.

Vuvuzela zimejipatia umaarufu mkubwa katika fainali za kombe la Dunia huko Afrika Kusini ambapo watu wengi walivutiwa na mtindo wa ushangiriaji kwa kupuliza zumari hizo za plastiki ambapo baadhi ya watu walionesha kukerwa na ushangiriaji kwa kutumia vuvuzela.
Soma Zaidi ...

RWANDA YAKANUSHA INAWAANDAMA WAPINZANI

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Rwanda Louise Mushikiwabo,amekanusha kabisa kuhusika kwa serikali ya nchi yake katika mashambulio dhidi ya wapinzani watatu wa ngazi ya juu, akisema maafisa wa upelelezi na waandishi habari wanapaswa kuwasaka watu wanaojaribu kuzusha vurugu, kabla ya ya uchaguzi ujao wa rais.

Akizungumza katika mahojiano na Shirika la habari la Marekani ,Associated Press mjini New York, waziri huyo alisema huenda serikali yake haiwapendezi baadhi ya watu , lakini haina upumbavu wa kufanya kitendo cha aina hiyo wakati mmoja.

Wakosoaji wanadai kwamba serikali ya Rwanda inawaandama na kuwakandamiza wapinzani kabla ya uchaguzi huo tarehe 9 mwezi ujao, wakitaja juu ya kuuwawa kwa mwandishi habari, Jean-Leonard Rugambage na kiongozi mmoja wa upinzani Andre Kagwa Rwisereka, na pia kupigwa risasi Jenerali wa zamani wa jeshi la nchi hiyo Kayumba Nyamwasa anayeishi uhamishoni Afrka kusini.
Soma Zaidi ...

CLINTON AZITOLEA WITO SCOTLAND NA UINGEREZA


Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani, Hillary Clinton amezitolea wito serikali za Scottland na Uingereza kupitia upya uamuzi walioutoa mwaka uliopita wa kuachiwa huru kwa mtu pekee aliyehukumiwa kuhusika na shambulio la bomu mwaka 1988 dhidi ya ndege ya Marekani huko Lockerbie, Scottland.

Abdel Baset al-Megrahi, raia wa Libya alihusishwa na shambulio hilo la ndege ya abiria ya Pan Am lililowaua abiria 270. Bibi Clinton aliwaandikia barua maseneta wanne wa Marekani akisema kuwa alizitaka serikali hizo kupitia upya mazingira yaliyosababisha uamuzi huo kufikiwa. Al-Megrahi aliachiwa huru Agosti mwaka 2009 kwa misingi ya huruma kwa sababu alikuwa akiugua saratani ambayo madaktari walisema alikuwa na miezi mitatu tu ya kuishi.

Hata hivyo, bado yuko hai hadi sasa. Suala hilo huenda likajadiliwa katika mazungumzo na Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron na Rais Barack Obama wa Marekani katika mkutano wao wa leo pamoja na suala la kuvuja kwa kisima cha mafuta cha kampuni ya mafuta ya BP na vita nchini Afghanistan. Soma Zaidi ...

MAMBO YA BIG BROTHERS ALL STARS


Yale maisha ya siku 91 ndani ya jumba huko Afrika Kusini yajuilikanayo kwa jina la Big Brother All Stars yameanza rasmin siku ya jumapili ambapo washiriki wapatao 14 kutoka katika nchi hizo hizo 14 wameingia katika jumba hilo.

Kwa mara nyengine tena Tanzania imepata nafasi ya kuingiza mwakilishi wake ndani ya jumba hilo ambe kwake yeye hii itakua ni mara ya pili kushuriki shindano hilo nae ni Mwisho Mwampamba, ambapo kwa mara ya kwanza yalipoanzishwa mashindano hayo miaka 7 iliyopita alishiriki.

Lakini kwa upande wake Mwisho inaonekana kama hakuanza vyema maisha ya nyumbani humo kwani jana Jumatatu alipoitwa kwenye diary room Big Brother alimtaka ataje majina mawili ya watu ambao angependa kuwaning'iniza kwa ajili ya kutolewa ndani ya jumba hilo lakini mwisho alishindwa kutaja hata jina moja kwa kile alichodai kwamba hakua akijua jina la mshiriki hata mmoja aliyeko ndani ya jumba hilo.

Kutokana na sheria za nyumbani humo kitendo hicho cha Mwisho kutomtaja mtu yoyote kimepelekea yeye mwenyewe kujitundika na kusubiri kupigiwa kura na matokeo kutangazwa siku ya Jumapili, na kama akipata kura za kumtosheleza anaweza kubakia na kuendelea na maisha ya humo ndani, lakini kama hakupata kura za kutosha, siku ya Jumapili itakua ndio mwisho wa maisha ya humo ndani kwa mwakilishi huyo pekee kutoka Tanzania. Soma Zaidi ...

Monday, July 19, 2010

UKIMWI NA CHANJO

Kirusi cha ukimwi

Shamrashamra nyingi tulizisikia hivi karibuni pale watafiti wa NIH nchini Marekani walipotoa ripoti ambayo ni habari njema katika vita dhidi ya Ukimwi. Watafiti hawa wameeleza kuwa wamegundua chembechembe, yaani antibodies, zenye uwezo mkubwa wa kuzuia kirusi cha ukimwi (HIV) kuingia kwenye seli nyeupe za damu — kwa 90% — na hivyo kusitisha mazaliano ya HIV.

Pamoja na shamrashamra hizi, wengi wetu tukaanza kusikia habari potofu zikisambazwa na wanahabari Tanzania kuwa ‘Dawa ya Ukimwi yapatikana,’ na kusikia vijana wakianza kuongelea (labda kushangilia) ngono isiyo salama, πβ%ϕЖ&!!

Ukweli ni kwamba ‘dawa ya Ukimwi´ haijagunduliwa - bali huu ni mwanzo tu wa safari ndeeefu ya kufikia nia hiyo. Mwaka jana kulikuwa na mlipuko wa habari kama huu kuhusiana na chanjo ya HIV – ila angalau ile ilikuwa tayari katika utafiti wa clinical trial!


‘Twisheni’

* Sote tunafahamu kuwa miili yetu hutengeneza chembechembe dhidi ya virusi, bakteria, n.k mbalimbali na hivyo kusitisha ugonjwa wanaosababisha kuanza.

* Kirusi cha ukimwi kinauwezo wa kubadilika kwa kasi kubwa na kuzaliana kabla mwili haujatengeneza chembechembe thabiti kudhibiti mazaliano zaidi ya virusi – by the time chembechembe thabiti zikiwa tayari, kirusi nacho kinakuwa tayari kimezalisha copy nyingine nyingi tofauti (a rat race!).

* Ripoti hii mpya inaeleza ugunduzi wa chembechembe (VRCO1 na VRCO2) zenye uwezo maradufu wa kuzuia kuzaliana kwa HIV katika maabara. Chembechembe hizi zinagundua na kubana sehemu ya kirusi isiyobadilika (isiyo mutate), kwahivyo kuzuia HIV kupenya na kuzaliana ndani ya seli nyeupe za damu.

* Umuhimu wa ugunduzi huu umetokana na teknolojia mpya za molecular/computational/structural biology ambazo zilitumika ili ‘kuvua’ chembechembe hizi kutoka kwa wagonjwa wa ukimwi. Baada ya test kadhaa maabarani, ndipo chembechembe hizi zikaonyesha uwezo wake huo mkubwa wa kuzuia HIV.

Changamoto zilizopo sasa ni kufahamu: Je, chembechembe hizi zina uwezo wa kiasi gani kuzuia HIV katika mwili wa mnyama au binadamu? Pindi chanjo madhubuti itakapopatikana, chembechembe hizi zinaweza kuzalishwa kawaida mwilini na mtu yeyote asiyeathirika ili kumkinga na HIV? Ni kiasi gani cha chembechembe hizi zitahitajika kuzuia HIV kuzaliana mwilini kwa ajili ya matibabu ya wagonjwa (passive immunization)? Haya ni baadhi ya maswali jumuiya ya sayansi itakabiliana nayo baada ya ripoti hii. Safari bado ni ndefu, na ni miaka kadhaa mpaka tutakapoona chanjo madhubuti dhidi ya HIV. Ila, imani bado ipo.
Soma Zaidi ...

MAAZIMIO YA KONGAMANO KUHUSU KURA YA MAONI NA SERIKALI YA UMOJA W AKITAIFA LILILOFANYIKA KATIKA UKUMBI WA BAYTUL YAMIN ZANZIBAR, TAREHE 17-18 JUL 2010

Sisi Wazanzibari washiriki wa Kongamano kuhusu Kura ya Maoni na Serikali ya Umoja wa Kitaifa lililofanyika Zanzibar kuanzia tarehe 17-18 Julai 2010:

Tunawapongeza kwa dhati Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Shariff Hamad kwa kuweka mbele maslahi ya Zanzibar na kusahau siasa za chuki na uhasama baina ya vyama vyao viwili;

Tunaamini viongozi hao wawili wataingia katika vitabu vya historia na kukumbukwa milele na vizazi vya Taifa hili, kwamba ni kutokana na ujasiri wao ndipo Zanzibar kwa mara ya kwanza ikaacha kuwa mtumwa wa historia yake ya vurugu za kisiasa na uhasama usiokwisha;

Kwamba kutokana na msimamo wao usiotetereka, Zanzibar ya leo imejenga imani na kuanza kuona mwanga wa matumaini wa Zanzibar ya kesho yenye ustawi, mapenzi na mshikamano, Zanzibar yenye mvuto kwa Wana wa Zanzibar walio ndani na nje ya visiwa hivi vyenye rutba na zawadi kemkem kwetu kutoka kwa Muumba;

Kwamba washiriki wa Kongamano wanawapa hongera waheshimiwa Wawakilishi wote, wakiongozwa na Spika, Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho kwa kuungana pamoja kwa ajili ya nchi hii na kusahau tofauti zao za kisiasa katika kusimamia na kuelekeza namna ambavyo Maridhiano ya Viongozi wetu wakuu wa kisiasa yatakavyotekelezwa;

Basi kwa kuzingatia yote hayo sisi Washiriki wa Kongamano hili la Kura ya Maoni na Serikali ya Umoja wa Kitaifa

Tumeazimia kama ifuatavyo:
1.Tutafanya kila aina ya ushawishi wa halali kuhakikisha kwamba Wazanzibari wanafahamu maana ya Kura ya Maoni na Serikali ya Umoja wa Kitaifa ili wafanye maamuzi sahihi kwa ajili ya maslahi ya Zanzibar.

2.Tutawashajiisha Wazanzibari kujitokeza kwa wingi na kupiga kura ya NDIO siku ya tarehe 31 Julai 2010 ili kuwezesha Serikali ya Umoja wa Kitaifa kuundwa.

3.Kwamba kila Mzanzibari katika nafasi yoyote aliyonayo atumie Uzalendo wake kuwashawishi Wazanzibari wote wachaguwe amani na mshikamano kwa kupiga kura ya NDIO kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

4.Vyombo vya habari vitowe elimu ya kutosha juu ya umuhimu wa Kura ya Maoni na Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kuwashajiisha Wazanzibari kupiga kura ya NDIO siku ya Kura ya Maoni.

5.Asasi za kiraia pamoja na jumuiya za kidini lazima zishirikishwe katika mchakato mzima wa Kura ya Maoni na Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

6.Tunataraji Tume ya Uchaguzi, ambayo ina mamlaka ya kusimamia Kura ya Maoni, itaheshimu matakwa ya wapiga kura na kutofanya vitendo ambavyo vitaiondolea imani mbele ya macho ya Wazanzibari.

7.Tunawashauri viongozi wote wa kisiasa kuacha ushabiki na utashi wa kisiasa wa kibinafsi na kivyama na kuangalia mustakbal mwema wa Zanzibar.

8.Kwamba Zanzibar hii mpya katu isiwavumilie wote wenye nia ya kutaka kuturudisha katika siasa za chuki na uhasama.

9.Chama cha siasa chochote kitakachopata nafasi ya kuingia katika Serikali baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2010, lazima kiheshimu maamuzi ya Baraza la Wawakilishi kuhusu uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hiyo iwe moja katika ahadi zake wakati wa kampeni.

10.Vyombo vyote vya ulinzi vya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vya Serikali ya Mapinduzi viwe tayari kuilinda na kuitetea Serikali ya Umoja wa Kitaifa kwa hali yoyote na viache vitendo vya kujihusisha na siasa.

11.Mahkama Kuu ya Zanzibar iwezeshwe kifedha na kiutaalamu ili iweze kuwa ni muhimili mkuu wa demokrasia Zanzibar.

12.Elimu ya uraia (civic education) iendelee kutolewa hata baada ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa kuundwa ili kuendelea na utulivu na mshikamano wa kisiasa Zanzibar.

MUNGU IBARIKI ZANZIBAR

IMEPITISHWA ZANZIBAR HII LEO TAREHE 18 JULAI 2010.


Soma Zaidi ...

Sunday, July 18, 2010

WACHEZAJI WA UHOLANZI WAUAGA UKAPERA


Mchezaji wa Uholanzi anaecheza kwatika safu ya ulinzi John Heitinga amefunga ndoa na mwanamke anaejuilikana kwa jina la Sophie Cherlotte ambae alikua akiishi nae na kuzaa nae mtoto moja wa kike.

Heitinga na Shophie wamefunga ndoa siku ya Alhamis katika fukwe za Cap d'falco huko mjini Ibiza Uhispania.

Alipozungumza na mwandishi wa habari wa gazeti la De Telegraaf la Uholanzi Sophie alisema kwamba "John ndie ndoto yangu na kila mmoja wetu anajisikia vizuri sana". alisema Sophie huku akitokwa na machozi.

Bada ya ndoa hio kufungwa kulifanyika sherehe kubwa ambayo ndugu na jamaa wa pande zote mbili walihudhuria wakiwemo marafiki, ambapo sherehe hio ilijumuisha watu 130.

Miongoni mwa watu maarufu waliohudhuria sherehe hio ni pamoja na Rafael van der Vaart na mkewe Sylvie, Estelle Gullit, Frank de Boer na familia yake, Patty Brard na Gordon.

Lakini wachezaji wengi wa Uholanzi hawakuhudhuria harusi hio kutokana na wachezaji hao kuwepo mpumziko baada ya kumaliza kwa Kombe la Dunia.

Wakati huo huo mchezaji wa Uholanzi ambae alipata zawazi ya pili kwa uchezaji bora katika fainali za Kombe la Dunia Wensley Snijder nae amefunga ndoa na mchumba wake Yolanthe.

Snijder na Yolanthe wamefunga ndoa leo hii katika kanisa moja huko nchini Italy ambapo ndoa hio ilifanyika katika mila za Kitaliano na Kiengereza.

Ndoa hio pia ilionekana kama ni ya kifalme kwani wanandoa hao waliingia kanisani wakiwa katika gari la farasi ambalo liliendeshwa na farasi 6 na baadae ndani ya kanisa hio mtoto wa Snijder anaejuilikana kwa jina la jessey aliingia na kumletea babaake pete ya ndoa.


Soma Zaidi ...

DUNIA YAADHIMISHA SIKU YA KUZALIWA KWA MANDELA


Rais mstaafu wa Afrika Kusini Nelson Mandela leo anatimiza miaka 92, huku ulimwengu ukisherehekea kwa mara ya kwanza, "Siku ya Nelson Mandela Duniani" kwa heshima ya kiongozi huyo.

Viongozi wa kimataifa na watu wa kawaida nchini Afrika Kusini na nje ya nchi hiyo, wameahidi kujitolea kuhudumia jamii kwa dakika 67 katika ishara za kuadhimisha miaka 67 ya kiongozi huyo kushughulikia harakati za kisiasa.

Mwaka 2009, Umoja wa Mataifa uliamua kuitambua tarehe 18 Julai - siku alizozaliwa mzee Mandela, kama "Siku ya kimataifa ya Nelson Mandela" na itakuwa ikisherehekewa kote duniani. Kwa mujibu wa familia yake, kiasi ya watoto 100 kutoka vijiji vilivyo karibu na kule alikozaliwa, watakuwa nae leo hii.

Tangu kuondoka madarakani, Mandela amejitokeza hadharani mara chache tu. Juma lililopita alikwenda kwenye uwanja wa michezo wa Soccer City mjini Johannesburg, kuwapungia mkono mashabiki wa kandanda kabla ya kufunguliwa mchezo wa fainali wa Kombe la Dunia, lakini hakubakia kutazama mchezo kwa sababu ya hali yake dhaifu ya afya. Soma Zaidi ...

Friday, July 16, 2010

MAHAKAMA YA ICC YAMUACHIA HURU KIONGOZI WA WAASI KONGO

Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ya ICC yenye makao yake The Hague Uholanzi imeagiza kuachiliwa huru kwa Kiongozi wa zamani wa waasi wa Congo Thomas Lubanga. Mahakama hiyo ilisema hakuna haja ya kuendelea kumzuilia Lubanga, ambaye kesi dhidi yake ilisimamishwa wiki moja iliopita. Lubanga ambaye amekuwa kizuizini kwa miaka minne, alikuwa anakabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kivita.

Thomas Lubanga kiongozi wa zamani wa waasi nchini Congo alikuwa anakabiliwa na mashtaka ya Uhalifu wa kivita- kwa kuwasajili kwa nguvu watoto waliokuwa chini ya umri wa miaka 15- kujiunga na kundi lake la Union of Congolese Patriots kwa nia moja tu ya kulimaliza kabila hasimu katika vita vya mwaka 1998 hadi 2003 katika Jamhuri ya Kideomkrasia ya Kongo.



Lubanga ambaye kesi yake ilianza kusikizwa Januari mwaka jana- na kugonga vichwa vya habari kwa kuwa ndio ilikuwa kesi ya kwanza mbele ya Mahakama hiyo ya uhalifu huko the Hague Uholanzi- alionekana kupata afueni wiki iliopita, pale kesi dhidi yake iliposimamishwa. Mahakama hiyo ya ICC ilisema imesimamisha kesi dhidi ya kiongozi huyo wa zamani wa waasi kwa sababu upande wa mashtaka ulikataa kuwasilisha taarifa kwa mawakili wa mshtakiwa.

Suala hili la kubadilishana taarifa kati ya upande wa mashtaka na wanasheria wanaomwakilisha Lubanga limeleta utatanishi mkubwa, na lilikuwa sababu ya kucheleweshwa kuanza kwa kesi dhidi ya kiongozi huyo wa zamani wa waasi. Pia kumekuwa na mvutano kuhusu ushahidi uliopo dhidi ya mtuhumiwa huyo.

Hata hivyo Koti hiyo ya uhalifu ilisema agizo la kuachiliwa huru kwa Lubanga halitatekelezwa mara moja, kwa sababu wanataraji upande wa mashtaka utakata rufaa katika siku tano zijaazo. Na naam kabla ya wino wa majaji hao kukauka Kiongozi wa Mashataka wa mahakama hiyo Louis Moreno Ocampo alitangaza atakata rufaa dhidi ya uamuzi wa kumuachilia huru Lubanga.

Vile vile Mahakama hiyo ilisema kuachiliwa huru kwa Lubanga kunategemea iwapo matayarisho yatakuwa yamekamilika ya kumsafirisha katika nchi ambayo itakuwa tayari kumpokea.

Lubanga amekuwa akizuiliwa tangu Machi mwaka 2006- kwa mashtaka ya uhalifu wa kivita nchini Kongo kwa kuwasajili vijana wadogo na kuwapa mafunzo ya kutekeleza mauaji na visa vingi vya ubakaji. Inasemekana Kiongozi huyo wa zamani wa waasi alikuwa anawasajili watoto wadogo wengine chini ya umri wa miaka kumi kutoka kabila la Hema ili kupigana na kabila hasimu la Lendu.

Wanasheria wanaomuakilisha Lubanga hata hivyo wameshikilia kuwa ushahidi dhidi ya mteja wao ilikuwa hila tupu.


Soma Zaidi ...

NYIMBO: Mrisho Mpoto ft Maunda Zoro Samahani Wanangu

Msikilize huyu msanii Mrisho Mpoto kwa kweli ni mtaalamu sana kwa mashairi, na mashairi yake yana maana ndani yake.

Soma Zaidi ...

Thursday, July 15, 2010

MAMBO YA USAFI YANAVYOPEWA UMUHIMU KWENYE NCHI ZA WENZETU

Gari hili ni maalum kwa kufagia pamoja kuzoa taka
Gari hii inafanya kazi ya kukosha uwanja

Leo nilipopita maeneo ya madukani katika kutafuta mahitaji ya kawaida nilipita sehemu hii ambayo kila siku ya Alhamis na Jumamosi kunakua soko la wazi na mara tu baada ya soko kufungwa huwa kunafanyika usafi wa hali ya juu ikiwa ni pamoja na kupita kwa gari la kufagia pamoja na kuoza taka zote na baadae linapita gari ambalo linakosha sehemu yote ambayo soko lilikua kama inavyoonekana kwenye picha, kwani wao wameweza wana nini na sisi tunashindwa tumekosa nini? Soma Zaidi ...

RAIS MUSEVEN ATAKA MAJESHI ZAIDI SOMALIA

Rais Yoweri Museveni wa Uganda ameelezea haja ya kuimarishwa kwa majeshi ya Afrika ya kulinda amani nchini Somalia na kufikia wanajeshi elfu 20 ili kuwateketeza wale wote waliyohusika na mashambulio ya mabomu mjini Kampala ambapo watu zaidi ya 70 waliauawa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika mji wa Ntungamo magharibi mwa Uganda, Rais Museveni amesema kuwa nchi yake inaweza kushiriki katika mpango huo wa kuwa na wanajeshi elfu 20 ambao watashirikiana na serikali ya mpito kuwateketeza magaidi.

Amesema mataifa ya Afrika Mashariki yamekubali kutuma wanajeshi wa ziada elfu mbili nchini Somalia, lakini baada ya tukio la Jumapili mjini Kampala,Rais Museveni amesema wanajeshi zaidi wanahitajika.

Kundi la Al Shaabab limedai kuhusika na shambulio hilo la mabomu na limetishia kufanya tena mashambulio kama hayo nchini Burundi.Burundi na Uganda ndiyo pekee zenye wanajeshi katika kikosi cha wanajeshi elfu sita cha Afrika cha kulinda amani nchini Somalia AMISOM.

Wakati huo huo kiongozi wa kundi la al-Shaabab Sheik Muktar Abu Zubayr amesema mashambulio hayo ya Uganda ni mwanzo tu na kwamba mashambulio zaidi yatafuatia. Soma Zaidi ...

RAIS MUSEVEN ATAKA MAJESHI ZAIDI SOMALIA

Rais Yoweri Museveni wa Uganda ameelezea haja ya kuimarishwa kwa majeshi ya Afrika ya kulinda amani nchini Somalia na kufikia wanajeshi elfu 20 ili kuwateketeza wale wote waliyohusika na mashambulio ya mabomu mjini Kampala ambapo watu zaidi ya 70 waliauawa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika mji wa Ntungamo magharibi mwa Uganda, Rais Museveni amesema kuwa nchi yake inaweza kushiriki katika mpango huo wa kuwa na wanajeshi elfu 20 ambao watashirikiana na serikali ya mpito kuwateketeza magaidi.

Amesema mataifa ya Afrika Mashariki yamekubali kutuma wanajeshi wa ziada elfu mbili nchini Somalia, lakini baada ya tukio la Jumapili mjini Kampala,Rais Museveni amesema wanajeshi zaidi wanahitajika.

Kundi la Al Shaabab limedai kuhusika na shambulio hilo la mabomu na limetishia kufanya tena mashambulio kama hayo nchini Burundi.Burundi na Uganda ndiyo pekee zenye wanajeshi katika kikosi cha wanajeshi elfu sita cha Afrika cha kulinda amani nchini Somalia AMISOM.

Wakati huo huo kiongozi wa kundi la al-Shaabab Sheik Muktar Abu Zubayr amesema mashambulio hayo ya Uganda ni mwanzo tu na kwamba mashambulio zaidi yatafuatia. Soma Zaidi ...

Wednesday, July 14, 2010

UNAIDS YATOA RIPOTI YAKE

Ripoti hiyo imeonyesha kuwa maambukizi ya virusi vya Ukimwi yamepungua hasa miongoni mwa vijana.

Shirika la Umoja wa Mataifa la kupambana na ugonjwa wa Ukimwi, UNAIDS limesema kuwa vijana barani Afrika wanaongoza katika mapinduzi ya kuzuia maambukizi ya virusi vya Ukimwi na Ukimwi kutokana kubadilika kitabia ikiwemo na kufanya ngono salama na kupunguza idadi ya wapenzi.

Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa hii leo na Shirika hilo la Umoja wa Mataifa la kupambana na ugonjwa wa Ukimwi, UNAIDS, maambukizi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Ukimwi yamepungua miongoni mwa vijana katika nchi 16 kati ya 25 ambazo ziliathiriwa vibaya na ugonjwa huo. Utafiti wa shirika hilo umebaini kuwa nyingi ya nchi hizo ziko katika nafasi nzuri ya kufanikiwa kupunguza maambukizi ya virusi vya Ukimwi na Ukimwi kwa asilimia 25 miongoni mwa vijana wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi 24, ifikapo mwishoni mwa mwaka huu. Ripoti hiyo imefafanua kuwa vijana wameweza kuonyesha kuwa wanaweza kuwa mawakala wa mabadiliko katika mapinduzi ya kuzuia maambukizi ya virusi hivyo.

Shirika hilo la Umoja wa Mataifa la kupambana na ugonjwa wa Ukimwi, UNAIDS, limezitaka nchi mbalimbali duniani kote kujifunza kutokana na mafanikio hayo na kuandaa mipango madhubuti kuhusu elimu ya afya na kujamiiana, uwepo wa vifaa vya kupima virusi vya Ukimwi na kupatikana kwa urahisi vifaa vya kuzuia maambukizo ya virusi hivyo kama vile condom za kiume. Inakisiwa kuwa vijana milioni tano duniani kote wenye kati ya umri wa miaka 14 hadi 24 wanaishi na virusi vya Ukimwi na karibu asilimia 80 ya vijana hao wanaishi katika eneo la kusini mwa jangwa la Sahara. Ripoti hii iliyotolewa kabla ya mkutano wa dunia utakaojadili ugonjwa wa Ukimwi wiki ijayo huko Vienna, imegundua kuwa kiwango cha virusi vya Ukimwi kimepungua miongoni mwa vijana katika nchi 16 kati ya 25 zilizoathiriwa vibaya na virusi hivyo, ikiwemo Kenya, ambako kumekuwa na mabadiliko ya asilimia 60 kati ya mwaka 2000 na 2005.

Ripoti hiyo imebainisha kuwa Botswana, Ivory Coast, Ethiopia, Kenya, Malawi, Namibia na Zimbabwe zote zimefanikiwa kufikia lengo lililokubaliwa mwaka 2001 la kupunguza maambukizi ya virusi vya Ukimwi kwa vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 24 kwa asilimia 25 ifikapo mwaka 2010.

Aidha, Burundi, Lesotho, Rwanda, Swaziland, Bahamas na Haiti pia ziko katika mwelekeo wa kulifikia lengo hilo. Utafiti wa shirika hilo umegundua kuwa chanzo kikubwa cha kupungua kwa maambukizi ya virusi hivyo ni vijana kubadilika kitabia.


Vijana katika nchi 13 kati ya 25 wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu kabla ya kujiingiza katika vitendo vya ngono na katika zaidi ya nusu ya nchi 25 vijana wamekuwa wakichagua kuwa na wapenzi wachache. Matumizi ya condom za kiume pia yamechangia kupungua kwa maambukizi hayo, huku nchi 10 zikiripotiwa kutumia zaidi condom hizo miongoni mwa wanawake, na nchi 13 condom hizo zikitumiwa zaidi na wanaume. Cameroon, Tanzania na Uganda zimeripotiwa kuongeza matumizi ya condom kwa wanawake na wanaume. Mwezi Novemba mwaka uliopita Shirika la Umoja wa Mataifa la kupambana na ugonjwa wa Ukimwi, UNAIDS, lilikadiria kuwa kiasi watu milioni 33.4 duniani kote walikuwa wanaishi na virusi vya Ukimwi.
. Soma Zaidi ...

KIONGOZI WA UPINZANI AKUTWA AMEKUFA RWANDA

Mwili wa Makamu wa Rais wa chama cha upinzani kisichosajiliwa nchini Rwanda cha Green Party Andre Kagwa Rwisereka, umekutwa karibu na gari lake wiki moja baada ya kutoweka kwake.

Polisi pamoja na chama hicho wamesema kuwa mwili wa kiongozi huyo ulikutwa kwenye eneo lenye maji karibu na mto Mukula kusini mwa mji wa Butare.

Msemaji wa polisi Eric Kayiranga amesema watu waliyomuona usiku kabla ya kutoweka wamesema alikuwa na fedha nyingi kwahivyo wanahisi huenda lilikuwa ni tukio la ujambazi.

Mwanzilishi wa chama hicho cha Democratic Green Party Frank Habineza amesema Rwisereka ulichinjwa,ingawaje kichwa kilibaki na mwili.

Chama cha Democratic Green kimeshindwa kupata usajili utakaokiwezesha kushiriki katika uchaguzi wa urais utakaofanyika mwezi ujayo.

Makundi yanayotetea haki za binaadamu yameilaumu serikali ya Rwanda kwa kukandamiza upinzani pamoja na vyombo vya habari kuelekea kwenye uchaguzi huo Soma Zaidi ...

Tuesday, July 13, 2010

FAINALI ZA KOMBE LA DUNIA BARANI AFRIKA LAZIUNGANISHA BARA ZIMA

Fainali za kwanza za kombe la dunia katika ardhi ya bara la Afrika zilipaswa kuionyesha dunia sura mpya ya bara hilo.

Ulikuwa mwezi mzima uliojaa shauku, maamuzi mabaya, shangwe nyingi, lakini ulikuwa pia mwezi uliojaa matumaini makubwa. Fainali za kwanza za kombe la dunia katika bara la Afrika, ilikuwa ishara ya matarajio makubwa katika bara hilo. Dunia ilipaswa kuona , kuwa Afrika kusini inatayarisha vizuri mashindano haya, na Waafrika walipaswa kwa ujumla kuzihimiza timu zao kusonga mbele.

Lakini mashindano ya kombe la dunia kweli yalistahili kuliunganisha bara lote na kusafisha haiba yake? Kombe la dunia ni nafasi kubwa kuweza kusafisha sura ya bara letu tukufu.

Kwa Joseph kutoka Cameronn fainali za kombe la dunia nchini Afrika kusini sio tu mchezo katika viwanja. Kijana huyo mchuuzi anazungumzia kile Waafrika wengi wanachofikiri. Haijawahi kutokea mashindano kama hayo ya kandanda kuwa na umuhimu mkubwa. Kutoka katika historia ya kutokuwa na chochote, amesema rais wa zamani wa Afrika kusini Thabo Mbeki. Katika fainali hizi za kombe la dunia mtu anaweza kukumbuka jambo moja, furaha ya Waafrika, na dhahiri ni ishara ya mapambano dhidi ya umasikini uliolizingira bara hilo kwa karne kadha pamoja na mizozo.

Sio tu Afrika kusini inaona mafanikio hayo ya kispoti kwa shauku kubwa. Bali pia nchi nyingine za bara hilo, zimeyaona mashindano hayo kuwa na umuhimu mkubwa.

Mafanikio haya yatalitumbukiza bara la Afrika katika hali mpya. Ni ahadi kwa mustakbali wa bara hilo.

Allah Anicet anaamini katika nguvu za michezo. Na pia ni makamu wa rais wa shirikisho la soka la Ivory Coast.

Michezo ina uwezo wa kuwaongoza raia. Na wale wote wasio wanasiasa. Michezo inatupa mtazamo wa pamoja sisi Waafrika. Kila mmoja hivi sasa anazungumzia kuhusu umoja wa nchi za Afrika na umoja wa Afrika. Na katika kiwango cha taifa michezo inaweza kuimarisha umoja wa kitaifa.

Hilo limeonyeshwa na Ghana , timu ya nchi hiyo ilipopambana hadi katika robo fainali. Kabla ya mchezo bara zima liliingiwa na homa, kuwaombea Black Stars kusonga mbele katika nusu fainali. Raia wa Afrika kusini waligawa bendera za Ghana bure na gazeti la Daily Sun , liliandika, Matumaini ya Afrika na ndoto yanatuwana kwa Black Stars.

Diego Forlan , mshambuliaji wa Uruguay, anakiri kwa usahihi, Tunalazimika kukabiliana na bara zima la Afrika. Na kwa wakati fulani hali ilionekana wazi, kila mmoja alikuwa na matamanio ya umoja wa Afrika nzima. Iwapo ni Ivory Coast, Cameroon ama Ghana, shauku ilikuwa haina mipaka, kama ilivyo mara zote, tangu Afrika kushiriki kwa mara ya kwanza katika fainali za kombe la dunia.

Tangu nchi ya kwanza kuwahi kufanikiwa kushiriki katika fainali za kombe la dunia, ikiwa ni Morocco mwaka 1970, kila timu ya Afrika inayofanikiwa kuingia katika fainali hizo inakuwa mwakilishi wa bara zima la Afrika.

Abdulrazak Abdulkarim , kocha na mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Ghana anaelezea kuwa,

Hatimaye watu katika bara zima la Afrika wanafurahia kandanda la Afrika. Hii ni hali nzuri kwetu sisi na hali nzuri kwa wachezaji wetu wachanga.

Nae Charles Adou, mwenye duka la dawa mjini Abidjan nchini Ivory Coast, anasisitiza jukumu walilolitekeleza timu ya Ghana katika fainali hizi za kombe la dunia, kwa kusema katika mazingira magumu Waafrika wamekuwa wapiganaji. Kama tulivyoona, vile Ghana ilivyofikia, kila mmoja alipaswa kuiunga mkono Ghana , kwamba ni timu ya kwanza , kutoka bara la Afrika kuingia nusu fainali.

Lakini ghafla, Ghana ilishindwa katika mikwaju ya penalti dhidi ya Uruguay. Na ndio timu ya mwisho ya Afrika kuondolewa katika fanali hizi za kombe la dunia.
. Soma Zaidi ...

Monday, July 12, 2010

TUNZO ZA ADIDAS KWA MASHINDANO YA KOMBE LA DUNIA

Mshambuliaji wa timu ya taifa ya Uruguay Diego Forlan ametajwa kua ndio mchezaji bora FIFA kwenye michuano ya kombe la dunia huko Afrika Kusini na kutunukiwa mpira wa dhahabu.
Forlan ametunukiwa tunzo hio ambayo inatolewa na kampuni ya Adidas baada ya kuisaidfia timu yake ya Uruguay kwa kuipatia jumla ya magoli matano na kufanikiwa kuingia katika nne bora.

Diego Forlan pia alitajwa katika jumla ya wachezaji wanaowania tunzo ya kiatu cha dhahabu, tunzo ambayo imekwenda kwa mchezaji wa taifa la ujerumani Thomas Muller.

Mchezaji wa pili aliyemfuatia Forlan ni Mchezaji kutoka timu ya taifa ya Netherlands "Oranje" Wensley Snijder ambae aliibuka na mpira wa fedha wakati mshambuliaji David Villa aliibuka na mpira wa shaba kwa kushinda nafasi ya tatu.
Soma Zaidi ...

WATU 23 WAFA KWA MIRIPUKO KAMPALA

Milipuko imetokea katika mji mkuu wa Uganda Kampala iliyolenga mashabiki wa soka waliotizama mechi ya fainali ya kombe la dunia katika televisheni.

Idadi kamili ya waliofariki bado haijulikani japo awali miili 23 ilipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti. Duru zinaarifu kuwa idadi hiyo inahofiwa kufikia zaidi ya watu 60.

Mkuu wa polisi nchini humo Kale Kaihura amesema kuwa uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa milipuko hiyo iliyotokea katika mikahawa ya vyakula na pombe ilinuiwa kusababisha maafa zaidi, ambapo mripuko wa kwanza ulitokea kwenye mgahawa wa Kiethiopea kusini mwa mji huo mkuu, na mripuko mwengine ulitokea kwenye mgahawa wa klabu ya mchezo wa Rugby mashariki mwa Kampala.

Shaka kuu imetiliwa kikundi cha wapiganaji wa kiislamu Al-Shabab nchini Somalia ambako Uganda imetuma majeshi yake kusaidia katika shughuli ya amani chini ya muungano wa Afrika

. Soma Zaidi ...

Sunday, July 11, 2010

MAMBO YA WAZUNGU



Picha hizi nilizipiga kipindi cha baridi na ilikua ni mwezi wa Januari mwaka huu, kwa wakati ule hapa palikua na uwanja wa mpira pamoja na mabenchi ambayo watu walikua wakikaa kipindi cha jua,lakini jamaa wameibadilisha hii sehemu na huwezi ukajua kama mwanzo hapa palikua hivi, picha za chini zinaonesha jinsi hali ya sasa uwanjani hapa ilivyo.

Hivi ndivyo hali ilivyo kwa sasa, hakuna tena uwanja wa mpira wala mabenchi ya kukalia, lakini jamaa wameweka mto wa maji ambao haukuwepo kabla, na wanatengeneza sehemu ya kuchezea watoto ambayo bado haijamaliza, uwanja huu ingelukua ni nyumbani basi wakubwa weshauchukua na kujijengea majumba yao binafsi, lakini kwa wenzetu wanajua ni jinsi gani ya kuwaridhisha wananchi wao na kujenga nchi yao, sijui hawa viongozi wetu wakija huku ulaya kila siku wanajifunza nini. Soma Zaidi ...

NYUMBA INAUZWA MOMBASA ZANZIBAR

Nyumba hii inauzwa ipo maeneo ya Mombasa karibu na skuli ya SOS na ipo karibu na barabara kuu ya kwa Mchina inayoelekea kiembe samaki, nyumba ina vyumba vitatu na chumba kimoja cha "master bed room", nyumba hii inauzwa sh 55Milioni, kwa maelezo zaidi wasiliana na Salum Humoud kwa simu nambari +255 774 309 094. Soma Zaidi ...

Saturday, July 10, 2010

KIJUA KIKIWAKA KILA MTU NA BALAA LAKE



Leo kijua kikiwa kimeaka kweli kweli jamaa walikua wakifanya mazoezina mziki Soma Zaidi ...

JUMAPILI TULIVU NA MAANDAZI

Leo niliyakumbuka maandazi na nikaona niyatengeze, na nilipoakanda unga haichukua hata dakika 20 yaliumuka. Soma Zaidi ...

MIFUKO YA PLASTIKI ZANZIBAR

Mfanya biashara ya machunga akiwa amefunga machungwa katika mifuko ya plastiki, mifuko ambayo nilisikia kwamba imepigwa marufuku Zanzibar, sasa je habari hizi zina ukweli wowote? na kama zinaukweli ndani yake kwa nini watu bado wanaitumia? Soma Zaidi ...

Friday, July 9, 2010

LEBRON JEMS KUHAMIA MIAMI HEAT MSIMU UJAO

Mcheza kikapu Nyota wa Marekani LeBron Jems ameamua kuachana na timu yake ya Cleverland na kuungana na rafiki yake Dwyane Wade kwenye timu ya Miami Heat, Jems alitangaza azma yake hio wakati alipozungumza kwenye chanali ya national television siku ya alkhamis. Soma zaidi >>> Soma Zaidi ...

Thursday, July 8, 2010

TUJIULIZE TUNAENDE WAPI?

Assalam aleykum

Tumetekwa na Ajenda za Siasa huku tukisahau wajibu wetu kuwatumikia Binadamu wenzetu khasa kuwapatia hifadhi Mayatima na Masikini.Nafasi ya kumtafuta nani awe mgombea imekuwa Muhimu zaidi ya kumtafuta nani wa kutunza Zakaah ili iwafikie Walengwa.

Pamoja na kuwa na UISLAAM zaidi ya Miaka elfu na ushee leo hii bado tunashindwa kuusimamisha kwa Vitendo Zanzibar. Wengine wakitafuta mbuzi wa kafara toka Dini zengine kuwasingizia Matatizo yetu ,wengine wakiwapachika mzigo huu wana Siasa wa Chama hichi au kile na kudhani kuna Chama fulani ndo jibu la Matatizo yetu.

Tukumbuke jibu la Umasikini wetu tunalo wenyewe,Jibu la kukosa Haki za Binadamu tunalo wenyewe na pia jibu la elimu Duni tunalo wenyewe. Tumekuwa Wateja wa itikadi za mivutano badala ya kuwa wenye Hisa kwenye Nchi yetu.

Tujiulize tunaenda wapi?

Zanzibar Zindabaad!

AMUR
. Soma Zaidi ...

HOTUBA YA RAIS MTARAJIWA MH. MOHAMMED YUSSUF

Hotuba iliyotolewa kwa waandishi wa Habari na Bwana Muhammad Yussuf kuelezea azma yake ya kutaka kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi katika ukumbi wa EACTROTANAL siku ya Alkhamisi tarehe 24 Juni 2010

SOMENI KWA FURAHA!!

AMUR

Ndugu Wana-habari,Wazanzibari wenzangu,Mabibi na Mabwana, Kwanza, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kunipa nguvu, afya njema na uhai wa kuwepo hapa leo. Pia napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Chama Cha Mapinduzi kwa kunipa fomu hii adhimu inayonipatia nafasi ya kuwa mmoja wa wagombea wa nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.

Kama tujuavyo, kipindi cha pili na cha mwisho cha uongozi wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Amani Abeid Amani Karume, kitamalizika mnamo mwezi Oktoba 2010. Kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar, Mheshimiwa Karume hatoweza tena kugombea kipindi kingine cha miaka mitano. Katika hali hii, ni jambo la kawaida kabisa kujitokeza wana-CCM wengine wengi tu kugombea nafasi itakayowachwa wazi na Mheshimiwa Rais Karume. Na vile vile, ni jambo la kupongezwa kabisa kuona kuwa mara hii jumla ya wana-CCM 11 wamejitokeza kuwania nafasi ya urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama chetu; mimi nikiwa mmoja miongoni mwao.

Huu ni uthibitisho tosha na wa dhahiri kuwa Chama cha Mapinduzi kinaheshimu misingi ya demokrasia ya kweli ndani yake yenye lengo la kuwapa fursa wanachama wake kugombea nafasi yoyote katika chama na serikali zake. Ni kutokana na hali hii basi, na kwa madhumuni ya kutumia haki yangu ya kidemokrasia kwa mujibu wa katiba ya chama chetu na ile ya Zanzibar, ndiyo sababu ya kwanza iliyonisukuma kuchukua fomu kugombea nafasi hii katika uongozi wa taifa letu.

Kwa hivyo, kati ya wanachama wetu hao 11, Hamlashauri Kuu ya Taifa itamteua mgombea mmoja tu miongoni mwao kukiwakilisha chama chetu katika uchaguzi ujao. Napenda kukiri kwa dhati kabisa kuwa wagombea wote hao ni wazuri na wenye kila sifa zifaazo, uwezo na uzoefu wa kutosha, kwa mujibu wa katiba ya chama chetu na katiba ya Zanzibar, kushika wadhifa wa urais wa Zanzibar. Hii inamaanisha kuwa sifa za wagombea sote sisi sio jambo la mjadala mkubwa; kwani sote ni wanachama hai wa chama chetu na wengine wameshikilia nyadhifa mbali mbali katika chama na serikali kwa muda mrefu na kujulikana sana. Mimi sijapata kushika wadhifa wowote ule wa uongozi katika chama; lakini nimeshika nyadhifa mbali mbali katika serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Maelezo zaidi yamo katika CV yangu.

Lakini, kutoshika wadhifa wowote ule wa uongozi katika chama hauninyimi sifa za kugombea wadhifa wa Urais wa Zanzibar. Kwa mujibu wa katiba ya CCM, inatosha tu, pamoja na sifa nyingine, kuwa mwanachama hai wa CCM, kugombea wadhifa wowote ule katika uongozi wa chama na/au serikali.

Kwa hivyo, jambo la msingi hapa sio kukimbilia Ikulu kwa sababu au mapenzi tu ya kutaka wadhifa wa Urais; bali ni kupata mgombea, sio tu atakayekiwezesha chama chetu kushinda katika uchaguzi ujao, bali la muhimu zaidi ni kupata mgombea mwenye uwezo, upeo na ubunifu wa sera na mikakati mizuri ambayo utekelezaji wake utaweza kuiletea nchi yetu maendeleo makubwa ya kiuchumi.

Hata hivyo, napenda kuahidi kuwa mgombea mwingine yoyote yule miongoni mwetu atakayebahatika kuteuliwa na chama chetu kugombea wadhifa wa Urais wa Zanzibar asiyekuwa mimi, basi nitampongeza kwa dhati kabisa na kushirikiana naye kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa anakiwezesha chama chetu kushinda katika uchaguzi ujao. Nasema hivi kwa sababu mchakato wa kumpata mgombea anayefaa kukiwakikisha chama chetu ni jambo la kidemokrasia kwa misingi ya ushindani na wala sio uadui wa kisiasa. Kadri chama kinapopata wagombea wengi wenye ujuzi na uzoefu tofauti ndivyo ambavyo chama kinavyopata upeo mpana wa kuteua mgombea anayefaa. Wakati wa kutafuta mgombea kwa njia ya mizengwe na usiri mkubwa umepitwa na wakati na hauna tena nafasi katika karne hii ya 21.

Katika kulizingatia hili kwa makini, Halmashauri Kuu ya Taifa, bila ya shaka yoyote ile, italazimika kumteua mgombea mwenye uwezo na ubunifu mkubwa katika jitihada za kuleta maendeleo makubwa nchini. Kutokana na elimu, uwezo na uzoefu mkubwa nilioupata katika utumishi wangu wa zaidi ya miaka 40 katika Serikali, katika medani ya kitaifa na kimataifa, nina kila sababu ya kuamini kuwa Zanzibar inahitaji kiongozi mwenye elimu, uwezo na uzoefu wa aina yangu ili kuiwezesha nchi yetu kupiga hatua kubwa sana kimaendeleo, kiuchumi, kijamii na hata kisiasa. Na hii hasa ndio sababu yangu ya pili iliyonisukuma kuamua kugombea wadhifa wa Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi.

Kwa lugha nyingine, wakati wa kulipa fadhila nilizopewa na wananchi wa Zanzibar, tokea kunisomesha mpaka kufikia mafanikio makubwa niliyoyapata katika maisha yangu umefika. Nasema hivi kwa sababu ikiwa mtoto niliezaliwa katika familia ya kimasikini, kama walivyokuwa wazee wangu wote, nimeweza kufanikiwa kuboresha maisha yangu kwa kiasi nilichonacho, basi nina kila sababu ya kuamini kuwa mtoto yoyote wa kimasikini anaweza kuboresha maisha yake ilimradi tu ikiwa atapatiwa fursa na nafasi za kujiendeleza na kuzitumia ipasavyo kama nilivyofanya mimi. Katika Zanzibar yenye kujali maslahi ya watu wake, mtu hapaswi kutoka katika familia ya kitajiri ili kufanikiwa. Kinachohitajika ni nia ya kujituma kwa vitendo, kutumia fursa zilizopo na kufanya kazi kwa bidii.

Kwa hivyo, katika kuthibitisha uwezo na uzoefu wangu huo, napenda kutumia nafasi hii, kuelezea kwa uwazi na ufasaha mkubwa nini nanakusudia kufanya katika kuiletea Zanzibar maendeleo ya kweli na endelevu ikiwa nitateuliwa na chama changu kugombea na hatimaye kuchaguliwa na wananchi kushika wadhifa wa Urais wa Zanzibar. Naamini kwa dhati kabisa kuwa kiongozi wa kweli ni yule mwenye uwezo wa kuitoa nchi yake katika dimbwi la umasikini uliokithiri na kuiingiza katika bwawa la utajiri na neema. Kwa mnasaba huu basi, nimeamua kujitosa moja kwa moja katika kinyang’anyiro cha kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar ili niwatumikiye Wazanzibari kwa madhumuni ya kufanikisha mambo muhimu makubwa kama hivi ifuatavyo:

1) Haja ya kuondokana na uhasama, chuki na mfarakano baina ya Waunguja na Wapemba

Ndugu Wananchi,
Ndugu Wana-habari,

Katika kipindi karibu chote cha utawala wa Rais Karume, kwa bahati mbaya, chuki, uhasama na mfarakano miongoni mwa wananchi wetu katika visiwa vyetu vya Unguja na Pemba, bado ulizidi kuhatarisha usalama, amani na mshikamano wa kitaifa katika nchi yetu. Kama alivyowahi kusisitiza Mwenyekiti wa chama chetu, Mheshimiwa Jakaya Kikwete, “mpasuko wa kisiasa” baina ya wananchi wa visiwa vyetu viwili bado ulikuwa ni suala sugu ambalo lilipaswa kupatiwa ufumbuzi wa kudumu haraka iwezekanavyo. Kwa bahati nzuri, Wazanzibari wengi tumefarijika kuona kuwa suala hili, hivi karibuni tu, limepatiwa ufumbuzi mzuri baada ya Rais Karume na Maalim Seif kufikia maridhiano yenye lengo la kuundwa kwa serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya Uchaguzi Mkuu mnamo mwezi wa Oktoba. Bila ya shaka yoyote ile, hii ni nafasi moja nzuri sana na ya kipekee ambayo, kama itatumiwa ipasavyo, basi uhasama, chuki na mfarakano baina ya wananchi wetu utakuwa ni jambo la historia.

Napenda kutumia fursa hii kuwapongeza viongozi hao wawili kwa ujasiri wao huo na kuahidi kuwa ikiwa nitachaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar, basi nitaendeleza kwa vitendo yote yale yaliyokubaliwa ikiwa ni pamoja na kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya kura ya maoni. Pia, naahidi kuwa tokea sasa ninaunga mkono wazo la kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na nakusudia kujenga hoja na kutumia ushawishi wangu kuwashawishi wapiga kura kupiga kura ya ndio. Pamoja na ukweli kuwa kura ya maoni inawapa fursa wananchi kutumia haki yao ya kikatiba kulitolea uamuzi suala hili, lakini papo hapo kiongozi muadilifu ana jukumu la kusaidia katika kuonyesha njia kwa kuwaelimisha wananchi juu ya hasara na faida zitakazopatikana kwa kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Kwa lugha nyingine, faida za kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ni kubwa zaidi kwa maslahi ya nchi yetu na Wazanzibari kwa jumla kuliko hasara zitakazopatikana nayo.

Kwa hivyo, ikiwa Halmashauri Kuu ya Taifa itaniteua mimi kuwa mgombea wa urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, basi katika kampeni za uchaguzi zitakazofuatia uteuzi wangu, nitaahidi na kusisitiza juu ya umuhimu na ulazima wa kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, sio tu baina ya CCM na CUF, bali vile vile pamoja na kuvishirikisha vyama vingine vyote vitakavyoshiriki katika uchaguzi ujao ilimradi tu navyo viwe vimepata viti katika Baraza la Wawakilishi. Hii inatokana na ukweli kuwa bila ya usalama, amani na mshikamano wa kitaifa, hakuna maendeleo yoyote yale yatakayoweza kupatikana nchini. Hili ni jambo la kwanza kabisa nitakalolitekeleza kama Rais wa Zanzibar ikiwa CCM itashinda katika uchaguzi ujao na wananchi walio wengi watapiga kura za ndio kwa madhumuni ya kuundwa kwa SUK.

Hata hivyo, napenda kutanabahisha jambo moja muhimu katika kuzingatia mustakbal wa Zanzibar baada ya kuundwa kwa SUK. Suala kubwa ambalo wananchi tunapaswa kujiuliza ni hili: Jee, baada ya kuundwa SUK nini kitafuatia baada yake? Inafaa kujiuliza hivi kwa sababu haitoshi tu kuwaingiza katika serikali viongozi wa vyama vya upinzani kwa sababu au mapenzi tu ya kushiriki katika shughuli za uendeshaji serikali; hasa kwa kuzingatia ukweli kuwa kuushirikisha upinzani katika serikali kunamaanisha kuupoteza upinzani wenyewe katika kutekeleza jukumu lake muhimu la kuimurika na kuikosoa serikali. Hii ni hatari kubwa sana kwa uhai wa demokrasia ya kweli yenye lengo la kuendeleza misingi madhubuti ya uwajibikaji na utawala bora.

Kwa hivyo, kuna haja ya kuhakikisha kuwa SUK itakayoundwa baada ya Uchaguzi Mkuu ujao itakuwa ni serikali ya muda mfupi tu kwa madhumuni ya kujenga misingi ya kuaminiana na kuweka mazingira mazuri ili chaguzi zifuatazo zifanyike katika mazingira ya uwazi kabisa, uhuru na haki; kwani, kwa bahati mbaya, hali hii hasa ndio chimbuko la mizozo ya kisiasa isiyokwisha nchini kwetu. Kama Rais wa Zanzibar, ninakusudia kuipitia katiba ya Zanzibar na Sheria zote za Uchaguzi nchini na kuzifanyia marekebisho yapasayo kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa chaguzi zote zinazofuata zinafanyika katika mazingira ya uwazi, uhuru na haki kabisa.

2. Haja ya kudumisha Muungano bila ya kudhoofisha mamlaka ya Zanzibar kwa mujibu wa katiba zetu zote mbili.

Ndugu Wananchi,
Ndugu Wana-habari

Kama tujuavyo, Muungano wa Tanzania bado unaendelea kukaribisha malumbano na manung’uniko yasiyokwisha baina ya pande zetu mbili hadi hii leo miaka 46 tokea kuanzishwa kwake. Kwa hivyo, ninaahidi kuzishughulikia kero za Muungano na kuzimaliza katika kipindi cha miaka mitano ya kwanza kwa kupendekeza marekebisho ya katiba zetu zote mbili kama vile ipasavyo.

Napenda kutanabahisha hapa kuwa kuimarisha Muungano haina maana hata kidogo ya kuingiza kila kitu katika orodha ya mambo ya Muungano. Nasema hivi kwa sababu ni ukweli usiofichika kuwa Muungano utaimarika zaidi ikiwa hatua za makusudi zitachukuliwa kuyaondoa yale mambo yote yaliyomo katika orodha ya Muungano ambayo upande mmoja wa Muungano unaamini kuwa kuendelea kubakia kwake hakuleti faida wala maslahi mazuri kwake na hivyo kuna muelekeo wa kuuathiri vibaya upande wake. Hili halina mjadala ikiwa dhana ya kuanzishwa kwa Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar imejengeka kikweli kweli katika misingi ya usawa, uhuru na upendo tokea hapo awali.

Isitoshe, inafaa kukumbusha hapa kuwa utaifa wa Tanzania unapata uhalali wake zaidi kutokana na mambo matatu ya msingi: uraia, mambo ya nje, na ulinzi na usalama. Nasisitiza hapa kuwa haya ni mambo ya kikatiba na ya msingi kabisa katika utaifa wa Tanzania. Bila ya ushirikiano wa kudumu baina ya Tanganyika na Zanzibar katika masuala haya matatu hapana shaka yoyote ile kuwa Muungano utavunjika. Na kwa vyovyote vile iwavyo, hakuna ushahidi wowote ule wa kuonesha kuwa manung’uniko makubwa ya Watanzania kwa jumla, na hasa zaidi ya Wazanzibari, yanatokana na mambo matatu haya.

Lakini, ni dhahiri kuwa mambo mengine yote yaliyomo katika orodha ya Muungano ni masuala ya kisera tu ambayo kuondolewa kwake hakutoathiri hata kidogo utaifa wa Tanzania au kusababisha kuvunjika kwa Muungano.

Kwa hivyo, ikiwa Halmashauri Kuu ya Taifa itanichagua kuwa mgombea wa CCM katika uchaguzi ujao, nitawaahidi wananchi kwa jumla na hususan wapiga kura, kuwa iwapo nitachaguliwa basi nitaanzisha mjadala wa kina na endelevu baina ya SMZ na SMT kwa kutumia nguvu ya hoja kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa mambo yale 11 tu yaliyomo katika Makubaliano ya Muungano ya 1964 yanaendelea kubakia katika orodha ya mambo ya Muungano. Mambo mengine yote yaliyoingizwa hapo baadaye hayana budi kuangaliwa upya kwa madhumuni, sio tu ya kuondosha kero, bali hasa zaidi kuimarisha Muungano. Hata kuhusu yale mambo 11 ya Muungano ya awali, si vibaya hata kidogo nayo kuangaliwa upya kwa madhumuni ya kuleta maelewano na maridhiano mema baina ya pande mbili husika.

Kwa mfano, ni kweli kabisa kuwa suala la Mambo ya Nje na Ulinzi ni suala la Muungano tokea hapo awali; lakini, suala la Ushirikiano ya Kimataifa (International Cooperation) si suala la Muungano kwa mujibu wa Makubaliano ya Muungano ya 1964. Hili liliingizwa hapo baadaye; pengine kwa sababu tu lina uhusiano wa karibu na Mambo ya Nje ya nchi. Lakini, ni ukweli usiofichika kuwa Ushirikiano wa Kimataifa unahusika zaidi na Maendeleo ya Kimataifa (International Development). Na ndio maana nchi nyingi zilizoendelea, kama vile Marekani, Uingereza, Sweden, Canada, na kadhalika, zimeanzisha Taasisi au Wizara maalum zinazohusiana na Ushirikiano wa Kimataifa. Iweje, kwa hivyo, Zanzibar isiwe na Wizara yake maalum inayohusika na suala hili muhimu la Ushirikiano wa Kimataifa kwa madhumuni ya kujiletea maendeleo?

Kwa kweli, moja katika manung’uniko makubwa ya SMZ, ni suala ambalo linajikita zaidi na misaada ya kiuchumi na kimaendeleo; na ndio maana mara nyingi hutokea mivutano isiyo ya lazima baina ya pande zetu mbili za Muungano. Ili kuepukana na hali hii, Zanzibar inahitaji kuwa na uhuru wa kutosha kushirikiana na nchi, Taasisi au Jumuiya mbali mbali kwa madhumuni ya kufaidika moja kwa moja na misaada ya kiuchumi na kimaendeleo bila ya kuingiliwa na SMT kwa yale mambo yasiyokuwa ya Muungano.

Kwa mfano, hakuna sababu yoyote ile ya msingi ya kuizuia Zanzibar kujiunga na OIS – taasisi ambayo malengo yake makubwa yamejikita katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi zaidi kuliko ile dhana inayoashiria kuwa Jumuiya hii ni taasisi yenye lengo na madhumuni ya kueneza dini ya Kiislamu miongoni mwa wanachama wake. Uwanachama wa nchi kama vile Uganda, Mozambique, Gabon na nyingi nyinginezo zenye wananchi wengi wanaofuata madhehebu ya dini ya Kikristo katika Jumuiya hii, ni ushahidi tosha kuwa lengo kubwa la Jumuiya hiyo ni kuendeleza Mashirikiano ya Kiuchumi na Kimaendeleo na wanachama wake zaidi kuliko kitu kingine. Kwa hivyo, hakuna sababu ya kuendelea kuizuia Zanzibar kujiunga na Jumuiya hii ikiwa Tanzania inashindwa kwa sababu yoyote ile kujiunga nayo. Kama kiongozi wa Zanzibar nitaanzisha mjadala wa kina na SMT kwa kutumia nguvu ya hoja ili kuhakikisha kuwa Tanzania au Zanzibar inajiunga na OIS katika kipindi changu cha miaka mitano ya kwanza.

Kwa mnasaba huu basi, hakuna sababu yoyote ile ya kuizuia Zanzibar kujiunga na taasisi za kimataifa kama vile, UNESCO, FAO, WHO, WFP, IAEA, WMO, IFAD – taasisi ambazo malengo yake makubwa yamo nje ya masuala ya Muungano ikiwa Zanzibar inakusudia kufanya hivyo siku za mbele. Na wala hakuna sababu ya msingi ya kukhofia kuwa Muungano utavunjika ati tu kwa sababu Zanzibar imejiunga na taasisi kama hizo. Kinyume chake, kuna kila sababu ya kuamini kuwa ushawishi wa Tanzania katika medani ya kimataifa utazidi kuongezeka na kupanuka zaidi kwa sababu Tanzania itakuwa na kura mbili katika Jumuiya hizo; kama vile ambavyo USSR hapo zamani ilivyokuwa ikifaidika kwa kuziruhusu Ukraine na Belorussia kujiunga na Umoja wa Mataifa. Na kwa kweli sote tunaelewa fika kuwa Urusi haikusambaratika kwa sababu ya uwanachama wa nchi hizo katika Jumuiya ya Umoja wa Mataifa (UNO).

Kama hili halitoshi, kilio kingine kikubwa cha Wazanzibari kinaambatana na kushindwa kwa ZFA kujiunga na FIFA. Mimi naamini kwa dhati kabisa kuwa inawezekana kabisa kwa Zanzibar kujiunga na Shirika hili la Soka Duniani ikiwa tu ZFA yenyewe itajisafisha kiutendaji na kujitegemea yenyewe kimapato. Kinyume chake, chama cha mpira kilichobobea migogoro isiyokwisha na kilichokosa nidhamu ya hali ya juu katika utendaji na uongozi wake, hakina nafasi wala uwezo wa kuushawishi uongozi wa FIFA kukubali ombi lake la kujiunga na Shirika hilo.

Isitoshe, pamoja na mambo mengine muhimu, Serikali ya Zanzibar kwa kushirikiana na SMT itapaswa kubuni mkakati wa kidiplomasia ya hali ya juu kwa madhumuni ya kuishawishi FIFA kulikubali ombi la ZFA. Jazba, lawama na ukosefu wa maelewano baina ya ZFA na TFA – yote haya yana muelekeo wa kudumaza jitihada za ZFA katika kujiunga na FIFA zaidi kuliko kuisaidia kufanikisha lengo hilo. Kama Rais wa Zanzibar, nitabuni mkakati kabambe wa kidiplomasia ya hali ya juu, ikiwa ni pamoja na kuzishawishi nchi zenye ushawishi mkubwa sana katika uongozi wa FIFA, kama vile Uingereza, Ufaransa, Uswisi kwa kushirikiana na SMT, ili kuhakikisha kuwa ZFA inajiunga na FIFA katika kipindi changu cha miaka mitano ya kwanza cha uongozi wangu.

3. Haja ya kuboresha uchumi wa Zanzibar

Wazanzibari wezangu,

Hali ya uchumi wa Zanzibar bado hairidhishi pamoja na maendeleo ya wastani yaliyokwisha kupatikana. Kwa hivyo, kuna haja kubwa ya kuboresha uchumi wa Zanzibar kwa njia ya kuleta mabadiliko kwenye sekta muhimu kabisa za kukuza uchumi wetu kama vile utalii, kilimo, uvuvi, biashara na viwanda. Nitahakikisha kuwa ukuwaji wa sekta hizi unaendana sambamba na mabadiliko makubwa katika mfumo wa elimu; huduma za afya na ujenzi wa miundo mbinu na njia mbadala za kupata nishati.

Inasikitisha kuona kuwa sera zote za kuboresha uchumi (Utalii, Viwanda, na Biashara) katika miaka kumi iliyopita hazijapata utekelezaji wa nguvu kwa kiwango ambacho tungelitegemea. Hakukuwa na ufanisi wa kutosha katika utekelezaji wake, mapato na ajira iliyotarajiwa.

Kwa mfano, SMZ ilitangaza kuanzisha maeneo huru ya uchumi ili wawekezaji waingize rasilmali zao katika ujenzi wa viwanda kwa madhumuni ya kuongeza ajira na kipato kwa wananchi wetu. Maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa viwanda katika maeneo huru kule Fumba, ukiacha lile eneo la viwanda vidogo vidogo hapo Amani, hayakufanywa lolote. Utalii pia umekuwa ukivujisha mapato na kutoa sehemu ndogo tu ya ajira kwa Wazanzibari. Matokeo yake, Zanzibar bado inaendelea kukumbwa na ukosefu mkubwa wa ajira kwa Wazanzibari hasa vijana wetu.

Katika jitihada za kukabiliana na hili, ninakusudia kutoa kipaumbele kwa Wazanzibari katika soko la ajira katika sekta za utalii, biashara, viwanda na kilimo. Asiyekuwa Mzanzibari ataajiriwa ikiwa tu muajiri ameshindwa kupata Mzanzibari mwenye sifa zifaazo. Mipango maalumu itabuniwa na kutekelezwa ili kuhakikisha kuwa Wazanzibari wanapatiwa utaalamu wa kutosha katika fani mbali mbali ili waweze kutimiza masharti ya soko la ajira nchini kwa misingi ya ushindani.

Ili kuongeza mapato makubwa zaidi katika uchumi wetu, nitahakikisha kuwa Serikali inabuni vianzio vipya vya mapato katika sekta zote za uchumi wa Zanzibar. Moja katika mbinu nitazozitumia ni kuifanyia marekebisho sera ya misamaha ya kodi kwa madhumuni ya kuepukana na matumizi yake mabaya. Nitaiangalia upya Sheria ya ununuzi na uuzaji wa vifaa na mali za serikali (Procurement Act) kwa madhumuni ya kupunguza gharama za ununuzi wa vifaa na kuongeza mapato ya serikali yatayopatikana katika uuzaji wa mali zake; nitaondoa kabisa utaratibu wa kuuziana mali za serikali kwa upendeleo na bei poa. La muhimu zaidi, nitaipitia bajeti ya serikali kifungu hadi kifungu kwa madhumuni ya kufuta matumizi yote yasiyokuwa ya lazima na hivyo kuiwezesha serikali kupata mapato ya ziada yatokanayo na ufanisi na nidhamu ya kifedha katika utekelezaji wa miradi na matumizi ya fedha.

Isitoshe, nitazipiga mnada gari zote za serikali za kifakhari za aina ya PRADO ili kuhakikisha kuwa mawaziri na viongozi wengine wa idara za serikali na mashirika yake wanatumia gari za gharama ndogo, kama vile RAV4 na kadhalika. Katika serikali nitakayoiongoza, itakuwa ni marufuku kuendelea na utaratibu unaowaruhusu mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa maidara na mashirika mbali mbali ya serikali kuendesha gari za serikali kama mali zao binafsi. Magari yote ya serikali yatakuwa chini ya usimamizi wa PWD; na yataendeshwa na madereva wa serikali na kuhudumiwa na mafundi wa serikali. Utekelezaji wa sera hii utaipunguzia serikali matumizi makubwa yasiyo ya lazima, kama vile malipo ya lita 25 za petroli au dizeli kwa siku yanayotolewa kuwahudumiya viongozi hao. Mapato yatayopatikana na mnada wa magari hayo pamoja na mapato ya ufanisi huo (efficiency gains) yatatumika katika kuboresha huduma za afya na elimu.

4. Haja ya kuleta mabadiliko katika mfumo wa huduma za jamii - zikiwemo elimu; huduma za afya na pia kutafuta mbinu za kupata vianzio mbadala vya nishati

Ndugu Wana-Habari,

Elimu ndio ufunguo wa maisha na maendeleo endelevu. Pia tukumbuke kuwa elimu ya msingi na sekondari ni haki ya kila mtoto nchini. Hili ni lengo la Serikali ya Mapinduzi tokea kufanyika kwa Mapinduzi ya 1964. Ni jambo la kufurahisha sana kuona kuwa kiwango cha uandikishaji watoto katika skuli za msingi kinazidi kukua mwaka hadi mwaka. Lakini, ongezeko hili haliendani na idadi ya skuli za msingi na hivyo kusababisha watoto wengi kulazimika kusoma katika darasa moja. Kwa mfano, hivi sasa kuna baadhi ya skuli zinachukua hadi watoto 100 katika darasa moja. Nyingine zinalazimika kusomesha kwa zamu. Utaratibu huu unaathiri sana maendeleo ya kitaaluma kwa watoto hawa. Serikali nitakayoingoza mimi itahakikisha kuwa idadi ya wanafunzi katika darasa inapunguzwa hadi kufikia watoto 35 kwa darasa na kuondoa kabisa utaratibu wa kusoma kwa zamu ili kuwapa watoto nafasi ya kutumia utoto wao ipasavyo. Nasema hivi kwa sababu mtoto aliyecheza mchana kutwa na kulazimikakuanza masomo katika nyakati za jioni hawezi kujifunza ipasavyo.

Isitoshe, kwa bahati mbaya, kiwango cha elimu nchini kimeshuka sana katika kipindi cha miaka ya karibuni. Katika kurekebisha hali hii, ninakusudia kuboresha kiwango cha elimu nchini kwa kuongeza bajeti yake marudufu i.e. kutoka asilimia 18 hadi asilimia 25 ya bajeti ya serikali. Tutajenga maskuli ya kisasa ya kutosha badala ya kuendelea kujenga majengo ya skuli ya aina ya mabanda ya kuku; kuziingizia skuli zetu zote kompyuta na maktaba za kisasa; na kuyapa kipaumbele masomo/mafunzo ya sayansi na teknolojia; kuajiri walimu wa kutosha na kuwapa taaluma ipasayo na mishahara mizuri inayolingana na hadhi ya taaluma yao ili kukidhi ongezeko kubwa la wanafunzi na kuinua kiwango cha elimu katika skuli za msingi na sekondari.

Katika Sekta ya Afya, pamoja na mambo mengine mbali mbali, ninakusudia kuboresha afya ya jamii. Nitatowa kipaumbele katika jitihada za kutokomeza kabisa maradhi ya Malaria na udhibiti wa maradhi ya kuambukiza hasa ya Ukimwi. Nitahakikisha kuwa kunakuwepo uwiano mzuri wa utoaji wa huduma ya afya mijini na mashamba (yaani huduma bora za afya zisiwe mijini tu, lakini mashamba pia zipatikane). Nitazifanyia ukarabati na kuzipatia zana za kileo hospitali zetu zote zinazomilikiwa na serikali na kuhakikisha kuwa hospitali na kliniki za watu binafsi ziko katika hali nzuri na ya kuridhisha. Hatua za makusudi zitachukuliwa kuajiri madaktari na wakunga wenye sifa zifaazo na kuwapatia mafunzo zaidi kila ipasavyo ikiwa ni pamoja na kuwaongezea mishahara kulingana na hadhi ya taaluma zao na haja ya kukabiliana na hali ngumu ya maisha. Mipango maalumu itabuniwa ili kuhakikisha kuwa kila Mzanzibari anapatiwa bima ya afya ili, yeye pamoja na familia yake, aweze kupatahuduma bora za afya yake hapa hapa nchini na kumudu gharama za matibabu ambazo kila kukicha zinazidi kuongozeka.

5. Haja ya Kupatikana kwa Nishati Mbadala na Kuboresha Huduma za Maji Safi

Ukosefu wa kupatikana kwa nishati ya uhakika ni suala linaloendelea kuwa sugu mwaka hadi mwaka na hivyo kuendelea kuathiri vibaya sekta zote za uchumi wa taifa. Ukosefu wa umeme umeleta athari kubwa za kiuchumi ikiwemo viwanda kufungwa, kupanda kwa gharama za uendeshaji katika mahoteli ya kitalii; na mamia ya wajasiriamali kupoteza ajira na kipato.

Isitoshe, huduma za maji nazo bado haziridhishi hata kidogo na hivyo kusababisha uhaba mkubwa wa maji katika maeneo mengi wanayoishi wananchi; hasa zaidi katika majumba ya ghorofa na katika viwanda na shughuli nyingine za uchumi. Matatizo haya sugu katika sekta hizi mbili muhimu za uchumi wa taifa, kwa pamoja, yanazorotosha uchumi wa Zanzibar kwa kiasi kikubwa na kuathiri vibaya sana ukuaji wake.

Kwa kutilia maanani matatizo haya sugu, ikiwa nitachaguliwa, ninaahidi kuleta mabadiliko makubwa katika mfumo mzima wa huduma za sekta mbili hizi na hasa zaidi katika kufikiria uwezekano wa kutafuta vianzio mbadala vipya na vya uhakika vya nishati.

6. Haja ya kuleta mabadiliko katika mfumo wa ardhi na ujenzi

Mabibi na Mabwana,

Kuanzia miaka ya 1990, SMZ ilifanya mapitio ya sheria za ardhi ili kuhakikisha kuwa inawatambuwa wamiliki ardhi; ilitoa hati miliki na kuzirekodi ardhi za wananchi wote nchini. Kwa bahati mbaya, miaka ishirini imepita, inasikitisha kuona kuwa bado sheria hizi hazikutekelezwa vya kutosha; na ndio maana kumekuwa na uendeshwaji wa shughuli za ardhi zisizoridhisha. Hali hii, mbali ya uuzwaji wa viwanja kinyume na sheria, dhulma kubwa inaendelea kufanywa dhidi ya baadhi ya wenye ardhi zenye thamani kubwa, hasa katika maeneo ya vijiji vilivyo kando na bahari ambako utalii umeshamiri. Baya zaidi, hali hii imesababisha ujenzi wa ovyo katika miji yetu ya Unguja na Pemba.

Kwa madhumuni ya kukabiliana na hili, hatua zifaazo zitachukuliwa kusafisha miji yetu na kudhibiti ujenzi wa ovyo ikiwa ni pamoja na kuanzishwa na kutekelezwa kwa sera mpya ya mipango miji; nitapiga marufuku utoaji holela wa viwanja na kuhakikisha kuwa shughuli hizo zinatekelezwa na mamlaka moja tu nchini kote chini ya Wizara inayohusika badala ya utaratibu unaotumika hivi sasa ambapo Sheha, Diwani, Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa n.k. wanaonekanwa kuwa na mamlaka ya kutoa viwanja.

Isitoshe, kuna baadhi ya wananchi ambao, pengine kwa makusudi kabisa, wameshindwa kujenga katika viwanja walivyopatiwa na serikali kwa muda uliowekwa kwa mujibu wa sheria. Baadhi ya wananchi hao, wamekuwa wakijaribu kuviuza viwanja hivyo kwa mamilioni ya fedha. Hii si sawa hata kidogo; na ni hatari kwa maslahi mema ya nchi wetu. Kwa hivyo, serikali yangu itahakikisha kuwa wananchi hao wananyang’anywa viwanja hivyo na kupewa wananchi wasiokuwa navyo.

Ndugu Wana-habari,

Majumba mengi ya maendeleo yanayomilikiwa na serikali hivi sasa yapo katika hali mbaya; mengine kati ya yale yaliyotaifishwa yanaanguka na kuporomoka ovyo hasa wakati wa mvua za masika; na mengine yanauzwa na/au kukodishwa kwa upendeleo na bei poa. Ninakusudia kubuni sera maalumu yenye lengo la kuyafanyia ukarabati majengo yote yanayomilikiwa na serikali, na kuyauza kwa mnada yote yale yaliyo katika hali mbaya sana kwa wananchi watakaokuwa tayari kuyatengeneza kwa kuzingatia bei halisi katika soko la kuuziana majumba; badala ya kuuziana kwa njia za upendeleo na/au bei poa kama ifanyikavyo hivi sasa. Papo hapo, nitaangalia uwezekano wa kuanzisha Revolving Fund ya ujenzi wa nyumba kwa madhumuni ya kuwapatia wananchi mikopo itakayowawezesha kujenga nyumba za bei nafuu.

7. Vita dhidi ya ufisadi na rushwa

Ndugu Wananchi,

Ufisadi na rushwa ni adui mkubwa wa haki. Kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa wananchi wote bila ya ubaguzi wa aina yoyote ile, kuna haja kubwa ya kuendeleza vita dhidi ya ufisadi na rushwa kwa kasi na ari kubwa zaidi bila ya muhali. Kama Rais wa Zanzibar, nitahakikisha kuwa misingi ya maadili ya uongozi na uwajibikaji inafuatwa na kutekelezwa kikamilifu ikiwa ni pamoja na kuondokana na tabia mbovu ya kulindana. Nitaanzisha Kitengo Maalum cha Kudhibiti Rushwa na Ufisadi katika nchi. Utekelezaji wa mambo haya utasaidia kwa kiasi kikubwa sana kuirejeshea Serikali na chama heshima yake; na papo hapo kuvutia hisia, imani na nyoyo za wapiga kura na wananchi kwa jumla. Na huu hasa ndio msingi muhimu katika utekelezaji mzima wa siasa safi na utawala bora wenye muelekeo wa kukipendezesha chama chetu, serikali na viongozi wake kwa mtazamo wa wananchi kwa jumla.

8. Kipaumbele katika kuhifadhi mazingira

Ndugu zanguni,

Inafaa kuzinduana hapa kuwa Zanzibar, isipofanya tahadhari, kuna hatari kubwa ya kupoteza rasilimali zake, ikiwemo ardhi yenye rutuba, misitu na miti ya asili, wanyama, na maeneo ya uvuvi. Kusema kweli, vitu vyote hivyo, tayari, viko mbioni kutoweka kwa haraka. Kama kiongozi wa nchi, nitachukuwa hatua thabiti katika jitihada zetu za pamoja ili kuhakikisha kuwa Serikali inashirikiana na wadau mbali mbali katika kuendeleza, kukuza na kuhamasisha ushirikishwaji wa jumuiya zisizo za kiserikali na watu binafsi katika kulinda na kuimarisha uhifadhi wa mazingira.

9. Watu wenye ulemavu

Pamoja na jitihada zinazoendelezwa na SMZ zenye lengo na madhumuni ya kuwasaidia watu wenye ulemavu kukabiliana na ulemavu wao; bado watu wenye ulemavu wanaendelea kukabiliwa na matatizo makubwa katika jamii ya Wazanzibari hasa kwa kuzingatia ukweli kuwa hali ya mazingira ya maisha yao ya kila sibu bado hayaonekani kuwa ni ya kirafiki.

Kwa mfano, majengo yanayoendelea kujengwa nchini, bado hayazingatii mahitaji ya watu wenye ulemavu, kama vile kutiwa lifti, au njia maalumu zenye kuwawezesha kupanda na kushuka kwa urahisi. Mabarabara yanayojengwa nayo hayana njia maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu; taasisi nyingi za serikali na zisizo za kiserikali bado hazina watu wenye ujuzi wa kutumia alama maalum kwa watu wasioona, na wasiosikia. Kama rais wa Zanzibar, hatua za makusudi zitachukuliwa kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu wanapatiwa mahitaji yao ili kuwawezesha kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku. Lengo kubwa litakuwa ni kuwafanya watu wenye ulemavu wajihisi wako sawa na watu wengine wote bila ya kuonekana kubaguliwa kwa namna yoyote ile.

10. Utaratibu wa kuchagua viongozi katika Serikali ya Zanzibar

Ndugu wananchi na waandishi wa habari,

Utaratibu unaotumika hivi sasa wa kuwapata viongozi wa Zanzibar, hasa Rais wake, una mapungufu makubwa kwa kiasi ambacho kinawafanya Wazanzibari wengi kutoridhika nao. Napenda kusisitiza hapa kuwa, ikiwa chama chetu kinataka kuvutia hisia, imani na nyoyo za wapigwa kura kwa madhumuni ya kuungwa mkono kwa sauti kubwa, basi wananchi wa Zanzibar lazima waonekanwe kuridhika na utaratibu wa kuchagua viongozi wao. Kuna haja kubwa, kwa hivyo, ya kuondoa dhana ya muda mrefu iliyojengeka miongoni mwa Wazanzibari inayoashiria kuwa Tanzania Bara, na wala sio Zanzibar, ndio inayowachagulia Wazanzibari kiongozi wao; na hata kumg’oa aliye madarakani ikiwa hatakiwi.

Inafaa ifahamike hapa kuwa Urais wa Zanzibar si suala la Muungano; kwa hivyo, Wazanzibari wanapaswa kujiwekea utaratibu wao wenyewe utakaowaruhusu kuchagua viongozi katika ngazi zote za serikali bila ya kuingiliwa, kwa namna yoyote ile, na chama au taasisi za Tanzania Bara. Kwa mnasaba huo, kuna haja kubwa ya kuimarisha shughuli na majukumu ya Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu maamuzi makubwa yanayoihusu Zanzibar moja kwa moja kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa maamuzi au mapendekezo yanayotolewa na kamati hiyo kuhusu masuala yanayoigusa Zanzibar moja kwa moja yanaheshimiwa kwa vitendo. Na haya ndio hasa yaliyokuwa madhumuni ya msingi ya kuanzishwa kwa Kamati hiyo tokea hapo awali. Utekelezaji wake, kwa hivyo, utasaidia sana katika kujenga imani, hisia na nyoyo nzuri za wananchi kwa chama tawala na serikali yake. Ninakusudia kulishughulikia hili kwa kushirikiana na wenzetu wa Bara kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa maamuzi yote yanayoihusuZanzibar moja kwa moja yanafanywa na Wazanzibari wenyewe kupitia vyombo vinavyohusika. 11.

Hitimisho

Ndugu Wananchi,

Nimelazimika kuchukua muda mrefu kidogo kusoma hotuba hii kwa sababu ya umuhimu na unyeti wa uamuzi ambao Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM italazimika kuufanya katika zoezi hili zima la kumtafuta mgombea atakayefaa na hasa zaidi yule atakaye kihakikishia chama chetu ushindi katika uchaguzi ujao. Mimi si malaika, na si kweli hata kidogo kuwa nina majibu ya kila tatizo linaloikumba Zanzibar. Lakini, nina hakika kuwa nimejaribu angalau kuainisha kwa uwazi kabisa nini hasa matatizo ya Zanzibar kwa kadri niyaonavyo na jinsi ambavyo kiongozi ajaye atakavyo lazimika kuyashughulukia pindi akichaguliwa. Ozoefu wangu wa zaidi ya miaka 40 nilioupata katika utumishi wa Serikali ya Tanzania, SMZ na Umoja wa Mataifa umenisaidia sana katika kuyaona mambo kama nilivyoainisha hapa. Na huu hasa ndio uoni wangu kwa mnasaba wa mustakbali wa Zanzibar ya kesho ambao, ikiwa nitateuliwa kugombea urais wa Zanzibar, ninakusudia kuuingiza katika Ilani ya Uchaguzi wa 2010.

Hata hivyo, hapana shaka yoyote ile kuwa masuala mengi bado yanahitaji majibu. Kwa mfano, wapi nakusudia kupata fedha za kutosha kuiwezesha serikali kukabiliana na utekelezaji wa yote hayo niliyoyaeleza hapo awali? Ni vianzio vipya vipi vya mapato ninavyokusudia kuvianzisha kwa madhumuni ya kuongeza mapato ya serikali? Kitu gani kinachonifanya kuamini kuwa kero za Muungano zitapatiwa ufumbuzi wa kudumu mnamo miaka mitano ijayo ya kipindi cha kwanza cha urais wangu? Hivi kweli ufisadi na rushwa vitashughulikiwa ipasavyo katika uongozi wangu na hivyo kuhakikisha kuwa ushindi unapatikana dhidi ya vita hivyo? na mengine mengi.

Kusema kweli, mpaka hivi sasa sina majibu kamili ya masuala hayo; lakini ninajua fika na kuamini kwa dhati kabisa kuwa yote hayo yanawezekana. Nasisitiza: yote hayo yanawezekana kwa sababu kinachohitajika hapa ni fikra na mawazo mapya. Zanzibar inao wasomi na wataalamu wa kila fani waliopo ndani na nje ya nchi ambao wanaweza kutayarisha mipango kabambe itakayoweza kutukwamua kutoka katika hali mbaya ya kisiasa na kiuchumi tuliyonayo hivi sasa. Kinachokosekana ni nia njema na ujasiri wa kuwatumia wasomi na wataalamu wetu hao ipasavyo na kikamilifu bila ya kujihisi kuwa kwa kufanya hivyo tutadhoofisha umaarufu wetu au mamlaka yetu. Kwa lugha nyingine, kwanza tunapaswa sisi wenyewe kubadilika; na pili, tunapaswa vile vile kuleta mabadiliko makubwa na ya kweli katika mfumo mzima wa utawala.

Isitoshe, Zanzibar inaweza kujifunza sana kutokana na mafanikio makubwa ya kiuchumi na kimaendeleo yaliyopatikanwa katika nchi zinazoendelea kama vile South Korea, Singapore, China, Taiwan, Brazil, India, Indonesia, Mauritius na kadhalika. Kwa mfano, Hong Kong inaweza kabisa kuwa ndio kielelezo kizuri juu ya jinsi ambavyo mahusiano ya kiuchumi na kisiasa baina ya Zanzibar na Tanzania Bara yanavyoweza kuendelezwa kwa ufanisi mkubwa kwa misingi ya kuelewana, kusaidiana na kushirikiana. Ili iweze kupiga hatua kubwa kimaendeleo, Zanzibar lazima ibuni na kutekeleza mikakati itakayoiwezesha kushindana na nchi hizo katika uuzaji wa bidhaa zake katika soko la dunia. Kwa manasaba huo, Zanzibar haina budi kufufua viwanda vyake vilivyokufa na kuanzisha viwanda vipya ili iweze kuzalisha bidhaa mbali mbali na kuziuza ndani ya Tanzania na nchi za nje. Kwa kufanya hivyo, Zanzibar itaongeza mapato yake ya nje na hivyo kuiwezesha kuongeza ajira kwa wananchi wake nakutunisha mapato yao.

Kwa upande wa Muungano, sina budi kusema kuwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Jakaya Kikwete, hapana shaka yoyote ile kuwa hakuna kero isiyoweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu; ilimradi tu ikiwa tutajadiliana kwa kutumia nguvu ya hoja badala ya hoja ya nguvu; tena bila ya kusudio la kutaka kuuathiri vibaya au kuuhatarisha Muungano wetu. Hii ndio nia na msimamo, kama sikosei, wa Mwenyekiti wetu pale aliposema kwa yakini kuwa hakuna lisilojadilika.

Kwa bahati mbaya wengi wetu tumeshindwa kuitumia nia hii njema ya Mwenyekiti wetu na Rais wa Jamhuri ya Muungano ipasavyo na kikamilifu kwa kujenga hoja muwafaka katika jitihada zetu za pamoja za kufikia ufumbuzi wa kudumu. Badala ya kutatua kero za Muungano, tumeufanya Muungano kuwa ndio kero. Tumejikuta tuna ukosefu mkubwa wa nia njema na ujasiri wa kujenga hoja madhubuti ndani ya wakati unaofaa. Katika uongozi wangu, sitokua mpungufu wa nia njema na ujasiri wa kulishughulikia suala hili kwa kuitumia nia njema ya Mwenyeketi wetu ipasavyo na kikamilifu kwa madhumuni ya kuudumisha na kuimarisha Muungano wetu kwa kuzingatia maslahi ya pande zote mbili.

Kwa mfano, katika jitihada za kuleta mashirikiano ya karibu baina ya pande zetu mbili, Zanzibar inaweza kubuni mikakati ya makusudi yenye lengo la kuwekeza katika mashirika, mabenki au makampuni makubwa yaliyopo Tanzania Bara, kama vile CRDB, VODACOM, Kampuni za Migodi ya Dhahabu na Almasi, na kadhalika, kwa kununua hisa na hivyo kuiwezesha kuvuna mapato yatokanayo. Katika kufanya hivyo, Zanzibar inaweza kuitumia Ofisi yake iliyopo Dar es Salaam kikamilifu kwa madhumuni ya kufuatilia kwa ukaribu zaidi shughuli za mabenki, mashirika na makampuni yanayotia faida kibiashara na kupendekeza serikalini ipasavyo badala ya kujikita zaidi katika kuendeleza shughuli za kuomba misaada kutoka nchi wafadhili tu pekee. Kwa lugha nyingine, Zanzibar na Tanzania Bara zinahitaji kuendeleza mahusiano na mashirikiano mapya yenye kujikita zaidi katika kukuza na kuboresha chumi zao badala ya kuangaliya kila kitu kwa mtazamo wa kisiasa tu.

Namalizia kwa kusisitiza hivi: Naam, yote haya yanawezekana kabisa; kwa sababu ni vyema wote wale wenye mawazo na fikra za kizamani wakatanabahi kuwa Zanzibar ya 2010 haina budi kuongozwa na watu wenye fikra na mawazo mapya; na walio tayari kuleta mabadiliko makubwa na ya kweli katika mfumo mzima wa utawala. Kwa bahati mbaya, mawazo ya kizamani sio tu yamepitwa na wakati, lakini kubwa zaidi ni kuwa kuna hatari kwamba wimbi la mabadiliko ya kweli lina athari ya kuwaacha nyuma wote wale watakaopingana nalo.

Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.

. Soma Zaidi ...